Zaburi 73:13-28
Zaburi 73:13-28 BHN
Je, nimetunza bure usafi moyoni, na kujilinda nisitende dhambi? Mchana kutwa nimepata mapigo, kila asubuhi nimepata mateso. Kama ningalisema hayo kama wao, ningalikuwa mhaini miongoni mwa watu wako. Basi, nilijaribu kufikiria jambo hili, lakini lilikuwa gumu mno kwangu, mpaka nilipoingia patakatifu pako. Ndipo nikatambua yatakayowapata waovu. Kweli wewe wawaweka mahali penye utelezi; wawafanya waanguke na kuangamia. Wanaangamizwa ghafla, na kufutiliwa mbali kwa vitisho. Ee Bwana, uinukapo, wao hutoweka mara, kama ndoto wakati mtu anapoamka asubuhi. Nilipoona uchungu moyoni na kuchomwa rohoni, nilikuwa mpumbavu na mjinga, nilikuwa kama mnyama mbele yako. Hata hivyo niko daima nawe, ee Mungu! Wanishika mkono na kunitegemeza. Wewe waniongoza kwa mashauri yako; mwishowe utanipokea kwenye utukufu. Mbinguni, nani awezaye kunisaidia ila wewe? Na duniani hamna ninachotamani ila wewe! Hata nikikosa nguvu mwilini na rohoni, wewe, ee Mungu, u mwamba wangu; riziki yangu kuu ni wewe milele. Anayejitenga nawe, hakika ataangamia. Anayekukana, utamwangamiza. Lakini, kwangu ni vema kuwa karibu na Mungu, wewe Bwana Mwenyezi-Mungu ndiwe usalama wangu. Nitatangaza mambo yote uliyotenda!