Zekaria 9
9
Hukumu juu ya adui za Israeli
1Neno la unabii:
Neno la Mwenyezi Mungu liko kinyume na nchi ya Hadraki
na Dameski itakuwa mahali pa kupumzika,
kwa kuwa macho ya watu na ya makabila yote ya Israeli
yako kwa Mwenyezi Mungu;
2pia juu ya Hamathi inayopakana nayo,
juu ya Tiro na Sidoni,
ingawa wana ujuzi mwingi sana.
3Tiro amejijengea ngome imara,
amelundika fedha kama mavumbi,
na dhahabu kama taka za mitaani.
4Lakini Bwana atamwondolea mali yake
na kuuangamiza uwezo wake wa baharini,
naye atateketezwa kwa moto.
5Ashkeloni ataona hili na kuogopa;
Gaza atagaagaa kwa maumivu makali,
pia Ekroni, kwa sababu
matumaini yake yatanyauka.
Gaza atampoteza mfalme wake
na Ashkeloni ataachwa pweke.
6Wageni watakalia mji wa Ashdodi,
nami nitakatilia mbali kiburi cha Wafilisti.
7Nitaondoa damu vinywani mwao,
chakula kile walichokatazwa kati ya meno yao.
Mabaki yao yatakuwa mali ya Mungu wetu,
nao watakuwa viongozi katika Yuda,
naye Ekroni atakuwa kama Wayebusi.
8Lakini nitailinda nyumba yangu
dhidi ya majeshi ya wanyang’anyi.
Kamwe mdhalimu hatashambulia watu wangu tena,
kwa maana sasa ninawachunga.
Kuja kwa Mfalme wa Sayuni
9Shangilia sana, ee Binti Sayuni!
Piga kelele, Binti Yerusalemu!
Tazama, Mfalme wako anakuja kwako,
ni mwenye haki, naye ana wokovu,
ni mpole, naye amepanda punda,
mwana-punda, mtoto wa punda.
10Nitaondoa magari ya vita kutoka Efraimu
na farasi wa vita kutoka Yerusalemu,
nao upinde wa vita utavunjwa.
Atatangaza amani kwa mataifa.
Utawala wake utaenea kutoka bahari hadi bahari,
na kutoka Mto#9:10 yaani Mto Frati hadi mwisho wa dunia.
11Kwako wewe, kwa sababu ya damu ya agano langu nawe,
nitawaacha huru wafungwa wako
watoke kwenye shimo lisilo na maji.
12Rudieni ngome yenu, enyi wafungwa wa tumaini;
hata sasa ninatangaza kwamba
nitawarejesheeni maradufu.
13Nitampinda Yuda kama nipindavyo upinde wangu,
nitamfanya Efraimu mshale wangu.
Nitawainua wana wako, ee Sayuni,
dhidi ya wana wako, ee Uyunani,
na kukufanya kama upanga wa shujaa wa vita.
Mwenyezi Mungu atatokea
14Kisha Mwenyezi Mungu atawatokea;
mshale wake utamulika kama radi.
Bwana Mungu Mwenyezi atapiga tarumbeta,
naye atatembea katika tufani za kusini,
15na Mwenyezi Mungu, Mungu wa majeshi ya mbinguni atawalinda.
Wataangamiza na kushinda
kwa mawe ya kutupa kwa kombeo.
Watakunywa na kunguruma kama waliolewa mvinyo;
watajaa kama bakuli linalotumika kunyunyizia
kwenye pembe za madhabahu.
16Mwenyezi Mungu, Mungu wao, atawaokoa siku hiyo
kama kundi la watu wake.
Watang’ara katika nchi yake
kama vito vya thamani kwenye taji.
17Jinsi gani watavutia na kuwa wazuri!
Nafaka itawastawisha vijana wanaume,
nayo divai mpya vijana wanawake.
Iliyochaguliwa sasa
Zekaria 9: NENO
Kuonyesha
Shirikisha
Nakili
Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia
Neno: Maandiko Matakatifu™ NMM™
Hakimiliki © 2018, 2024 na Biblica, Inc.
Imetumiwa kwa ruhusa.
Haki zote zimehifadhiwa duniani kote.
Kiswahili Contemporary Scriptures™
Copyright © 2018, 2024 by Biblica, Inc.
Used with permission. All rights reserved worldwide.