Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Mathayo 3

3
Yahya atayarisha njia
(Marko 1:1-8; Luka 3:1-18; Yohana 1:19-28)
1Siku hizo Yahya alikuja akihubiri katika nyika ya Yudea, akisema, 2“Tubuni, kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.” 3Huyu ndiye yule aliyenenwa habari zake na nabii Isaya aliposema:
“Sauti ya mtu aliaye nyikani,
‘Itengenezeni njia kwa ajili ya Mwenyezi Mungu,
yanyoosheni mapito yake.’#3:3 Isaya 40:3
4Basi Yahya alivaa mavazi yaliyotengenezwa kwa singa za ngamia, akiwa na mkanda wa ngozi kiunoni mwake. Chakula chake kilikuwa nzige na asali ya mwitu. 5Watu walikuwa wakimwendea kutoka Yerusalemu, Yudea yote na nchi zote za kandokando ya Mto Yordani. 6Nao wakaziungama dhambi zao, akawabatiza#3:6 Ubatizo ni ishara ya kuungama dhambi na kusamehewa na Mwenyezi Mungu, na kuweka nadhiri ya kubadilisha mienendo ya awali. katika Mto Yordani.
7Lakini alipowaona Mafarisayo#3:7 Kundi la kidini la Wayahudi; walifuata Torati kwa dhati, hasa maagizo kuhusu utakaso. Pia waliamini katika malaika, ufufuo wa wafu, na kuja kwa Masihi ambaye atarejesha ufalme wa Daudi na ukuu wa taifa la Israeli. na Masadukayo#3:7 Kundi la kidini la Wayahudi; waliamini kwamba hakuna ufufuo, wala hakuna malaika au roho. wengi wakija ili kubatizwa, aliwaambia: “Ninyi watoto wa nyoka! Ni nani aliyewaonya kuikimbia ghadhabu inayokuja? 8Basi zaeni matunda yastahiliyo toba. 9Wala msidhani mnaweza kusema mioyoni mwenu kuwa, ‘Sisi tunaye Ibrahimu, baba yetu.’ Nawaambia kuwa Mungu anaweza kumwinulia Ibrahimu watoto kutoka kwa mawe haya. 10Hata sasa shoka limeshawekwa tayari katika shina la kila mti, basi kila mti usiozaa matunda mazuri, hukatwa na kutupwa motoni.
11“Mimi nawabatiza kwa maji kwa ajili ya toba. Lakini nyuma yangu anakuja yeye aliye na uwezo kuliko mimi, ambaye sistahili hata kuvichukua viatu vyake. Yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu wa Mungu#3:11 au katika Roho wa Mungu na kwa moto. 12Pepeto lake liko mkononi mwake, naye atasafisha sakafu yake ya kupuria, na kuikusanya ngano ghalani na kuyateketeza makapi kwa moto usiozimika.”
Isa abatizwa
(Marko 1:9-11; Luka 3:21-22)
13Kisha Isa akaja kutoka Galilaya hadi Mto Yordani ili Yahya ambatize. 14Lakini Yahya akajitahidi kumzuia, akimwambia, “Mimi ninahitaji kubatizwa na wewe, nawe waja kwangu nikubatize?”
15Lakini Isa akamjibu, “Kubali hivi sasa, kwa maana ndivyo itupasavyo kwa njia hii kuitimiza haki yote.” Hivyo Yahya akakubali.
16Naye Isa alipokwisha kubatizwa, mara alipotoka ndani ya maji, ghafula mbingu zikafunguka, akamwona Roho wa Mungu akishuka kama hua na kutulia juu yake. 17Nayo sauti kutoka mbinguni ikasema, “Huyu ni Mwanangu mpendwa; ninapendezwa sana naye.”

Iliyochaguliwa sasa

Mathayo 3: NENO

Kuonyesha

Shirikisha

Nakili

None

Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia