Isaya 53
53
1Ni nani aliyeamini ujumbe wetu,
na mkono wa Mwenyezi Mungu umefunuliwa kwa nani?
2Alikua mbele yake kama mche mwororo
na kama mzizi katika nchi kavu.
Hakuwa na uzuri wala utukufu wa kutuvutia kwake,
hakuwa na chochote katika sura yake cha kutufanya tumtamani.
3Alidharauliwa na kukataliwa na wanadamu,
mtu wa huzuni nyingi, ajuaye mateso.
Kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao,
alidharauliwa, wala hatukumhesabu kuwa kitu.
4Hakika alichukua udhaifu wetu
na akajitwika huzuni zetu;
tulidhania kuwa ameadhibiwa na Mungu,
naye akapigwa sana na kujeruhiwa.
5Lakini alijeruhiwa kwa ajili ya makosa yetu,
alichubuliwa kwa ajili ya maovu yetu;
adhabu iliyotuletea sisi amani ilikuwa juu yake,
na kwa majeraha yake sisi tumepona.
6Sisi sote, kama kondoo, tumepotea,
kila mmoja wetu amegeukia njia yake mwenyewe,
naye Mwenyezi Mungu aliweka juu yake
maovu yetu sisi sote.
7Alionewa na kuteswa,
hata hivyo hakufungua kinywa chake;
aliongozwa kama mwana-kondoo
apelekwaye machinjoni,
kama vile kondoo anyamazavyo mbele ya wao wamkataye manyoya,
hivyo hakufungua kinywa chake.
8Kwa kuonewa na kuhukumiwa aliondolewa.
Nani awezaye kueleza kuhusu kizazi chake?
Kwa maana alikatiliwa mbali na nchi ya walio hai,
alipigwa kwa ajili ya makosa ya watu wangu.
9Wakamfanyia kaburi pamoja na waovu,
pamoja na matajiri katika kifo chake,
ingawa hakutenda jeuri,
wala hapakuwa na hila kinywani mwake.
10Lakini yalikuwa ni mapenzi ya Mwenyezi Mungu
kumchubua na kumsababisha ateseke.
Ingawa Mwenyezi Mungu amefanya maisha yake
kuwa sadaka ya hatia,
ataona uzao wake na kuishi siku nyingi,
nayo mapenzi ya Mwenyezi Mungu
yatafanikiwa mkononi mwake.
11Baada ya maumivu ya nafsi yake,
ataona nuru ya uzima na kuridhika;
kwa maarifa yake, mtumishi wangu mwenye haki
atawafanya wengi kuwa wenye haki,
naye atayachukua maovu yao.
12Kwa hiyo nitamgawia sehemu miongoni mwa wakuu,
naye atagawana nyara pamoja na wenye nguvu,
kwa sababu aliyamimina maisha yake hadi mauti,
naye alihesabiwa pamoja na wakosaji.
Kwa kuwa alichukua dhambi za wengi,
na kuwaombea wakosaji.
Iliyochaguliwa sasa
Isaya 53: NENO
Kuonyesha
Shirikisha
Nakili
![None](/_next/image?url=https%3A%2F%2Fimageproxy.youversionapi.com%2F58%2Fhttps%3A%2F%2Fweb-assets.youversion.com%2Fapp-icons%2Fsw.png&w=128&q=75)
Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia
Neno: Maandiko Matakatifu™ NMM™
Hakimiliki © 2018, 2024 na Biblica, Inc.
Imetumiwa kwa ruhusa.
Haki zote zimehifadhiwa duniani kote.
Kiswahili Contemporary Scriptures™
Copyright © 2018, 2024 by Biblica, Inc.
Used with permission. All rights reserved worldwide.