YouVersion Logo
Search Icon

Mwanzo 32

32
1Asubui mapema Labani akaamuka, akawabusu wajukuu na wabinti zake, akawabariki. Kisha akaondoka, akarudi kwake.
Yakobo anajitayarisha kukutana na Esau
2Yakobo akaendelea na safari yake. Basi, wamalaika wa Mungu wakakutana naye. 3Yakobo alipowaona, akasema: “Hii ni kambi ya jeshi la Mungu!” Kwa hiyo akaita pahali pale “Kambi mbili”.
4Yakobo alituma wajumbe wamutangulie kwenda kwa ndugu yake Esau, kule Seiri, katika inchi ya Edomu. 5Akawapa maagizo haya: “Mutamwambia bwana wangu Esau hivi: Mutumishi wako Yakobo anasema hivi: ‘Nimekaa mugeni kwa Labani mpaka sasa. 6Nina ngombe, punda, makundi ya kondoo, watumwa na wajakazi. Ninakutumia ujumbe huu, bwana wangu, kusudi nipate kukubaliwa mbele yako.’ ”
7Hao wajumbe walikwenda, kisha wakarudi na kumwambia Yakobo: “Tumefika kwa ndugu yako Esau, naye yuko katika njia kuja kukupokea, akiwa na watu mia ine.”
8Basi, Yakobo akaogopa sana na kufazaika. Akawagawanya katika makundi mawili watu waliokuwa pamoja naye, kondoo, nyama wengine na ngamia, 9akifikiri: “Kama Esau akikuja na kuliangamiza kundi moja, basi, kundi litakalobaki litaponyoka.”
10Kisha Yakobo akamwomba Mungu akisema: “Ee Mungu wa babu yangu Abrahamu, Mungu wa baba yangu Isaka! Ewe Yawe uliyeniambia nirudi katika inchi yangu kwa jamaa yangu, ukaniahidi kunitendea mema, 11sistahili hata kidogo wema wote na uaminifu wote ulionitendea mimi mutumishi wako. Nilipovuka muto Yordani, sikukuwa na kitu isipokuwa fimbo; lakini sasa nina makundi haya mawili. 12Ninakuomba uniokoe sasa kutoka kwa ndugu yangu Esau, maana nina hofu kwamba atatushambulia na kutuua wote, mama pamoja na watoto. 13Wewe uliniahidi kunitendea mema na kuwafanya wazao wangu wakuwe wengi kama muchanga wa bahari ambao hauhesabiki kwa wingi wake.”
14Basi, Yakobo akalala pale usiku ule. Kisha akatenga sehemu ya mali yake, ikuwe zawadi kwa ndugu yake Esau: 15mbuzi dike mia mbili na mabeberu makumi mbili, kondoo dike mia mbili, na dume makumi mbili, 16ngamia makumi tatu wanaonyonyesha pamoja na watoto wao, ngombe dike makumi ine, ngombe dume kumi, punda dike makumi mbili, na dume kumi.
17Akawapatia watumishi wake, kila mumoja kundi lake, akawaambia: “Mutangulie mukiacha nafasi kati ya kundi na kundi katika mustari wenu.” 18Akamwagiza yule aliyetangulia: “Ndugu yangu Esau atakapokutana nawe na kukuuliza: ‘Wewe ni mutumishi wa nani? Unakwenda wapi? Na nyama hawa ni wa nani?’ 19Wewe utamujibu: ‘Hii ni mali ya mutumishi wako Yakobo, nayo ni zawadi yako wewe bwana wangu Esau. Tena Yakobo mwenyewe yuko nyuma anafuata.’ ” 20Akatoa agizo hilohilo kwa mutumishi wa kundi la pili na la tatu na wengine wote, akisema: “Mutamwambia Esau maneno hayohayo mutakapokutana naye. 21Zaidi ya yote, mutamwambia: ‘Mutumishi wako Yakobo yuko nyuma, anafuata.’ ” Yakobo alifanya hivyo akifikiri: “Pengine nitamutuliza kwa zawadi hizi ninazomutangulizia na kisha nitaweza kuonana naye macho kwa macho; labda atanipokea.” 22Basi, akatanguliza zawadi zake, lakini yeye mwenyewe akalala katika kambi usiku ule.
Mapigano usiku
23Usiku uleule Yakobo akaamuka, akatwaa wake zake wawili, wajakazi wake wawili na watoto wake kumi na mumoja, akapita kivuko cha Yaboki. 24Kisha kuwavukisha ngambo ya kijito wale waliokuwa nao na mali yake yote, 25Yakobo akabaki peke yake.
Kisha mutu mumoja akakuja, akapigana naye mpaka asubui. 26Mutu yule alipoona kwamba hawezi kumushinda Yakobo, alimugusa Yakobo kwenye maunganio ya kiuno, naye akateguka alipokuwa anapigana naye.
27Kisha yule mutu akamwambia Yakobo: “Uniache nijiendee, maana kunapambazuka.”
Lakini Yakobo akamwambia: “Sitakuacha hata kidogo, mpaka umenibariki!”
28Naye akamwuliza: “Jina lako nani?”
Yeye akamujibu: “Yakobo.”
29Yule mutu akamwambia: “Hautaitwa Yakobo tena, lakini Israeli,#32.29 Israeli: ni kama neno la Kiebrania lenye maana “anayepigana na” au: “Mungu anapigana”. kwa sababu umeshindana na Mungu na wanadamu, ukashinda.”
30Halafu Yakobo akamwambia: “Tafazali, ninakuomba uniambie jina lako.”
Lakini yeye akamwambia: “Kwa nini kuniuliza jina langu?” Kisha akamubariki Yakobo.
31Yakobo akaita pahali pale Penueli,#32.31 Penueli: ni kama neno la Kiebrania lenye maana “uso wa Mungu”. akisema: “Nimemwona Mungu uso kwa uso, nami sikukufa.” 32Jua lilikuwa limekwisha kupanda wakati Yakobo alipoondoka Penueli, akakuwa anachechemea kwa sababu ya kiuno chake. 33Ndiyo maana mpaka leo Waisraeli hawakuli mushipa wa maunganio ya kiuno, kwa maana yule mutu alimugusa Yakobo kwa maunganio katika mushipa wa kiuno chake.

Currently Selected:

Mwanzo 32: SWC02

Highlight

Share

Copy

None

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in