Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Zaburi 51:1-19

Zaburi 51:1-19 BHN

Nihurumie, Ee Mungu, kadiri ya fadhili zako; ufutilie mbali makosa yangu, kadiri ya wingi wa huruma yako. Unioshe kabisa hatia yangu; unisafishe dhambi yangu. Nakiri kabisa makosa yangu, daima naiona waziwazi dhambi yangu. Nimekukosea wewe peke yako, nimetenda yaliyo mabaya mbele yako. Uamuzi wako ni wa haki hukumu yako haina lawama. Mimi ni mkosefu tangu kuzaliwa kwangu, mwenye dhambi tangu tumboni mwa mama yangu. Wewe wataka unyofu wa ndani; hivyo nifundishe hekima moyoni. Unitakase kwa husopo, nitakate; unioshe niwe mweupe pe. Nijaze furaha na shangwe, nifurahishe tena, mimi ambaye uliniponda. Ugeuke, usiziangalie dhambi zangu; uzifute hatia zangu zote. Uniumbie moyo safi, ee Mungu, uweke ndani yangu roho mpya na thabiti. Usinitupe mbali nawe; usiniondolee roho yako takatifu. Unifanye nifurahi tena kwa kuniokoa, utegemeze ndani yangu moyo wa utii. Hapo nitawafunza wakosefu njia yako, nao wenye dhambi watarudi kwako. Uniokoe na hatia ya umwagaji damu, ee Mungu, Mungu mwokozi wangu, nami nitaimba kwa sauti kuwa umeniokoa. Uniwezeshe kusema, ee Bwana, midomo yangu itangaze sifa zako. Kwa kweli wewe hupendezwi na tambiko, ama sivyo mimi ningalikutolea. Wewe huna haja na tambiko za kuteketezwa. tambiko yangu kwako ee Mungu, ni moyo mnyofu; wewe, ee Mungu, hukatai moyo mnyofu na mtiifu. Ee Mungu, upende kuutendea mema mji wa Siyoni; uzijenge tena upya kuta za mji wa Yerusalemu. Hapo utapendezwa na tambiko za kweli: Sadaka za kuteketezwa na za kuteketezwa nzima; mafahali watatolewa tambiko madhabahuni pako.

Soma Zaburi 51

Mipango ya Kusoma Bila Malipo na Ibada zinazohusiana na Zaburi 51:1-19