Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

1 Mambo ya Nyakati 19:1-19

1 Mambo ya Nyakati 19:1-19 SRUV

Ikawa baada ya hayo, Nahashi, mfalme wa wana wa Amoni, akafa, akatawala mwanawe mahali pake. Naye Daudi akasema, Nitamtendea wema Hanuni, mwana wa Nahashi, kwa kuwa babaye alinitendea mimi wema. Basi Daudi akatuma wajumbe ili kumtuliza kwa habari za babaye. Wakaja watumishi wa Daudi katika nchi ya wana wa Amoni kwa Hanuni, ili wamtulize. Lakini wakuu wa wana wa Amoni wakamwambia Hanuni, Je! Unadhani Daudi amewatuma wafariji kwako kwa heshima ya baba yako? Je! Hawakukujia watumishi wake ili kuichunguza nchi, na kuiangamiza, na kuipeleleza? Basi Hanuni akawatwaa watumishi wa Daudi, akawanyoa, akawapasulia nguo zao katikati, hadi kiunoni, kisha akawaachilia waondoke. Ndipo wakaondoka. Watu walipomwambia Daudi jinsi wajumbe wake walivyotendewa, alituma watu kuwalaki; kwa sababu walikuwa wameaibishwa sana. Mfalme akasema, Ngojeni Yeriko, hadi mtakapoota ndevu zenu, ndipo mrudi. Na wana wa Amoni walipoona ya kuwa wamejisababishia machukizo kwa Daudi, Hanuni na wana wa Amoni wakatuma talanta elfu moja za fedha ili kukodi magari na wapanda farasi kutoka Mesopotamia, na kutoka Atam-maaka, na kutoka Soba. Basi wakakodi magari elfu thelathini na mbili, na mfalme wa Maaka na watu wake; nao walikuja wakatua mbele ya Medeba. Na wana wa Amoni wakakusanyika kutoka miji yao, wakaja vitani. Basi Daudi aliposikia habari akamtuma Yoabu, na jeshi lote la mashujaa. Wakatoka wana wa Amoni, wakajipanga kwa vita langoni pa mji; na hao wafalme waliokuja walikuwa peke yao uwanjani. Basi Yoabu alipoona ya kwamba wamejipanga kwa vita juu yake mbele na nyuma, akachagua baadhi ya wateule wote wa Israeli, akawapanga juu ya Washami. Na hao watu waliosalia akawatia mikononi mwa Abishai, nduguye, nao wakajipanga juu ya wana wa Amoni. Akasema, Washami wakiwa ni hodari mno kwangu, ndipo wewe utanisaidia; lakini wana wa Amoni wakiwa ni hodari mno kwako, ndipo mimi nitakusaidia wewe. Kuwa hodari, tuwe na ujasiri, kwa ajili ya watu wetu, na kwa ajili ya miji ya Mungu wetu; naye BWANA afanye yaliyo mema machoni pake. Basi Yoabu, na watu waliokuwa pamoja naye, wakakaribia kupigana na Washami; nao wakakimbia mbele yake. Na wana wa Amoni walipoona ya kwamba Washami wamekimbia, wakakimbia nao mbele ya Abishai, nduguye, wakaingia mjini. Ndipo Yoabu akaja Yerusalemu. Na Washami walipojiona kuwa wameshindwa mbele ya Israeli, wakatuma wajumbe, wakawaleta Washami walioko ng'ambo ya Mto, na Shobaki, jemadari wa jeshi la Hadadezeri, akawaongoza. Alipoambiwa Daudi; akakusanya Israeli wote, akavuka Yordani, akawajia, akapanga vita juu yao. Basi Daudi alipopanga vita juu ya Washami, wakapigana naye. Washami wakakimbia mbele ya Israeli; naye Daudi akawaua katika Washami watu wa magari elfu saba, na askari waendao kwa miguu elfu arubaini, akamwua na Shobaki, jemadari wa jeshi. Na watumishi wa Hadadezeri walipojiona kuwa wameshindwa mbele ya Israeli, walifanya amani na Daudi, wakamtumikia; wala Washami hawakukubali kuwasaidia wana wa Amoni tena.