Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

1 Mambo ya Nyakati 14:1-17

1 Mambo ya Nyakati 14:1-17 SRUV

Naye Hiramu, mfalme wa Tiro, akatuma wajumbe kwa Daudi, akampelekea na mierezi, na waashi, na maseremala, ili wamjengee nyumba. Daudi akajua ya kwamba BWANA amemweka imara ili atawale Israeli, na kwamba milki yake imetukuka zaidi kwa ajili ya watu wake Israeli. Tena Daudi akazidi kuoa wake huko Yerusalemu; akazidi kuzaa wana na binti. Na haya ndiyo majina ya watoto aliozaliwa huko Yerusalemu; Shamua, na Shobabu, na Nathani, na Sulemani; na Ibhari, na Elishua, na Elpeleti; na Noga, na Nefegi, na Yafia; na Elishama, na Eliada, na Elifeleti. Wafilisti waliposikia ya kwamba Daudi ametiwa mafuta ili awe mfalme wa Israeli wote, Wafilisti wote wakapanda kumtafuta Daudi; naye Daudi akasikia, akatoka nje kupigana nao. Basi hao Wafilisti walikuwa wamekuja na kujitawanya katika bonde la Warefai. Daudi akamwuliza Mungu, akisema, Je! Nipande juu ya Wafilisti! Utawatia mikononi mwangu? Naye BWANA akamwambia, Panda; kwa kuwa nitawatia mikononi mwako. Basi wakapanda mpaka Baal-perasimu, Daudi naye akawapiga huko; Daudi akasema, BWANA amewafurikia adui zangu kwa mkono wangu, kama mafuriko ya maji. Basi wakapaita mahali pale jina lake Baal-perasimu. Nao wakaiacha miungu yao huko; naye Daudi akaamuru, ikateketezwa kwa moto. Lakini hao Wafilisti wakajitawanya tena mara ya pili bondeni. Na Daudi akamwuliza Mungu tena; naye Mungu akamwambia, Hutapanda kuwafuata; zunguka mbali nao, na kuwajia ukielekea miforsadi. Kisha itakuwa utakapoisikia sauti ya kwenda katika vilele vya miforsadi, ndipo utakapokwenda nje vitani; kwa maana ndipo Mungu ametoka mbele yako, awapige jeshi la Wafilisti. Daudi akafanya kama vile Mungu alivyomwamuru; wakawapiga jeshi la Wafilisti toka Geba mpaka Gezeri. Sifa za Daudi zikafika nchi zote; naye BWANA akawaletea mataifa yote hofu yake.

YouVersion hutumia vidakuzi kubinafsisha matumizi yako. Kwa kutumia tovuti yetu, unakubali matumizi yetu ya vidakuzi kama ilivyoelezwa katika Sera yetu ya Faragha