Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Lk 8:4-15

Lk 8:4-15 SUV

Mkutano mkuu ulipokutanika, na wale waliotoka kila mji wakimjia, alisema kwa mfano; Mpanzi alitoka kwenda kupanda mbegu zake; naye alipokuwa akizipanda, nyingine zilianguka karibu na njia, zikakanyagwa, ndege wa angani wakazila. Nyingine zikaanguka penye mwamba; zilipoanza kumea zikakauka kwa kukosa rutuba. Nyingine zikaanguka kati ya miiba, na miiba ikamea pamoja nazo ikazisonga. Nyingine zikaanguka penye udongo mzuri; zikamea, zikazaa moja kwa mia. Alipokuwa akinena hayo alipaza sauti akisema, Mwenye masikio ya kusikilia, na asikie. Wanafunzi wake wakamwuliza, Maana yake nini mfano huo? Akasema, Ninyi mmepewa kuzijua siri za ufalme wa Mungu; bali wengine kwa mifano, ili wakiona wasione, na wakisikia wasielewe. Na huo mfano, maana yake ni hii; Mbegu ni neno la Mungu. Wale wa karibu na njia ndio wasikiao, kisha huja Ibilisi akaliondoa hilo neno mioyoni mwao, wasije wakaamini na kuokoka. Na wale penye mwamba ndio wale ambao wasikiapo hulipokea lile neno kwa furaha; nao hawana mizizi, huamini kitambo kidogo, na wakati wa kujaribiwa hujitenga. Na zilizoanguka penye miiba ni wale waliosikia, na katika kuenenda kwao husongwa na shughuli na mali, na anasa za maisha haya, wasiivishe lo lote. Na zile penye udongo mzuri, ndio wale ambao kwa unyofu na wema wa mioyo yao hulisikia neno, na kulishika; kisha huzaa matunda kwa kuvumilia.

Soma Lk 8

Mipango ya Kusoma Bila Malipo na Ibada zinazohusiana na Lk 8:4-15