Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Yer 11:1-17

Yer 11:1-17 SUV

Neno hili ndilo lililomjia Yeremia, kutoka kwa BWANA, kusema, Yasikieni maneno ya maagano haya; ukaseme na watu wa Yuda, na wenyeji wa Yerusalemu; ukawaambie, BWANA, Mungu wa Israeli, asema hivi, Na alaaniwe mtu asiyeyasikia maneno ya maagano haya, niliyowaamuru baba zenu, siku ile nilipowatoa katika nchi ya Misri, katika tanuru ya chuma, nikisema, Itiini sauti yangu, mkafanye sawasawa na yote niwaagizayo ninyi; ndivyo mtakavyokuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wenu; ili nipate kukitimiza kiapo nilichowaapia baba zenu, kuwapa nchi ijaayo maziwa na asali, kama ilivyo leo hivi. Ndipo nikajibu, nikasema, Amina, Ee BWANA. Naye BWANA akaniambia, Hubiri maneno haya yote katika miji ya Yuda, na katika njia kuu za Yerusalemu, ukisema, Yasikieni maneno ya maagano haya, mkayafanye. Kwa maana naliwashuhudia sana baba zenu, siku ile nilipowatoa katika nchi ya Misri, hata leo, nikiamka mapema na kuwashuhudia, nikisema, Itiini sauti yangu. Lakini hawakutii, wala kutega masikio yao, bali walikwenda kila mtu katika ushupavu wa moyo wake mbaya; kwa hiyo nimeleta juu yao maneno yote ya maagano haya, niliyowaamuru wayafanye; lakini hawakuyafanya. Naye BWANA akaniambia, Fitina imeonekana katika watu wa Yuda, na katika wenyeji wa Yerusalemu. Wameyarudia maovu ya baba zao, waliokataa kusikia maneno yangu; wamewafuata miungu mingine na kuwatumikia; nyumba ya Israeli, na nyumba ya Yuda, wameyavunja maagano yangu niliyoyafanya na baba zao. Basi, BWANA asema hivi, Tazama, nitaleta mabaya juu yao, ambayo hawataweza kuyakimbia; nao watanililia, walakini sitawasikiliza. Ndipo miji ya Yuda, na wenyeji wa Yerusalemu, watakwenda na kuwalilia miungu wawafukiziao uvumba; lakini hawatawaokoa hata kidogo wakati wa taabu yao. Maana hesabu ya miungu yako, Ee Yuda, ni sawasawa na hesabu ya miji yako; na kama ilivyo hesabu ya njia za Yerusalemu, ndivyo mlivyosimamisha madhabahu za kitu kile cha aibu, madhabahu za kumfukizia Baali uvumba. Basi, usiwaombee watu hawa, wala usipaze sauti yako, wala kuwaombea dua watu hawa; maana sitawasikia wakati watakaponililia kwa ajili ya taabu yao. Mpenzi wangu afanya nini nyumbani mwangu, ikiwa amefanya uasherati? Je! Nadhiri zako na nyama takatifu zitakuondolea hatia? Ufanyapo maovu, ndipo uonapo furaha. BWANA alikuita jina lako, Mzeituni wenye majani mabichi, mzuri, wenye matunda mema; kwa kelele za mshindo mkuu amewasha moto juu yake, na matawi yake yamevunjika. Kwa maana BWANA wa majeshi, aliyekupanda, ametamka mabaya juu yako, kwa sababu ya maovu ya nyumba ya Israeli, na ya nyumba ya Yuda, waliyoyatenda juu ya nafsi zao wenyewe kwa kunikasirisha, wakimfukizia Baali uvumba.

Soma Yer 11

YouVersion hutumia vidakuzi kubinafsisha matumizi yako. Kwa kutumia tovuti yetu, unakubali matumizi yetu ya vidakuzi kama ilivyoelezwa katika Sera yetu ya Faragha