Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

2 Sam 6:1-15

2 Sam 6:1-15 SUV

Basi Daudi akakusanya tena wateule wote wa Israeli, watu thelathini elfu. Akaondoka Daudi akaenda pamoja na watu wote waliokuwa naye, mpaka Baala wa Yuda, ili kulipandisha kutoka huko sanduku la Mungu lililoitwa kwa jina, naam, jina la BWANA wa majeshi akaaye juu ya makerubi. Wakaliweka sanduku la Mungu juu ya gari jipya, wakalitoa katika nyumba ya Abinadabu, iliyoko kilimani; nao Uza na Ahio wana wa Abinadabu wakaliendesha lile gari jipya. Wakalitoa katika nyumba ya Abinadabu iliyoko kilimani, pamoja na sanduku la BWANA; na huyo Ahio akatangulia mbele ya sanduku. Daudi na nyumba yote ya Israeli wakacheza mbele za BWANA kwa nguvu zao zote, kwa nyimbo, na kwa vinubi, na kwa vinanda, na kwa matari, na kwa kayamba, na kwa matoazi. Hata walipofika kwa uga ya Nakoni, Uza akalinyoshea mkono sanduku la Mungu, akalikamata kwa maana wale ng’ombe walikunguwaa. Ndipo hasira ya BWANA ikawaka juu ya Uza; naye Mungu akampiga huko kwa kosa lake; hata akafa pale pale penye sanduku la Mungu. Daudi akaona uchungu kwa kuwa BWANA amemfurikia Uza; akapaita mahali pale Peres-uza hata leo. Naye Daudi akamwogopa BWANA siku ile; akasema, Litanijiaje sanduku la BWANA? Basi Daudi hakutaka kulileta sanduku la BWANA kwake mjini mwa Daudi; ila Daudi akalihamisha nyumbani kwa Obed-edomu, Mgiti. Sanduku la BWANA akalitia katika nyumba ya Obed-edomu, Mgiti, muda wa miezi mitatu; naye BWANA akambarikia Obed-edomu, na nyumba yake yote. Kisha mfalme Daudi akaambiwa ya kwamba, BWANA ameibarikia nyumba ya Obed-edomu, na vitu vyote alivyo navyo kwa ajili ya sanduku la Mungu. Daudi akaenda, akalileta sanduku la Mungu, toka nyumba ya Obed-edomu mpaka mji wa Daudi, kwa shangwe. Hata ikawa, watu waliolichukua sanduku la BWANA walipokwisha kwenda hatua sita, akachinja ng’ombe na kinono. Daudi akacheza mbele za BWANA kwa nguvu zake zote; na Daudi alikuwa amevaa naivera ya kitani. Basi Daudi na nyumba yote ya Israeli wakalileta sanduku la BWANA kwa shangwe, na kwa sauti ya tarumbeta.

Soma 2 Sam 6

Mipango ya Kusoma Bila Malipo na Ibada zinazohusiana na 2 Sam 6:1-15