Zaburi 35
35
Zaburi 35
Kuomba msaada: Kuokolewa kutokana na adui
Zaburi ya Daudi.
1Ee Mwenyezi Mungu, pingana na wale wanaopingana nami,
upigane na hao wanaopigana nami.
2Chukua ngao na kigao.
Inuka unisaidie.
3Inua mkuki wako na fumo#35:3 Fumo ni sawa na sagai, yaani mkuki mfupi. lako
dhidi ya hao wanaonifuatia.
Iambie nafsi yangu,
“Mimi ni wokovu wako.”
4Wafedheheshwe na waaibishwe
wale wanaotafuta uhai wangu.
Wanaofanya shauri kuniangamiza
wafukuzwe mbali kwa bumbuazi.
5Wawe kama makapi yapeperushwayo na upepo,
malaika wa Mwenyezi Mungu akiwafukuza.
6Njia yao na iwe giza na ya utelezi,
malaika wa Mwenyezi Mungu akiwafuatilia.
7Kwa vile walinifichia wavu wao bila sababu,
na bila sababu wamenichimbia shimo,
8maafa na yawapate ghafula:
wavu walionifichia na uwatege wenyewe,
na waanguke katika shimo hilo,
kwa maangamizi yao.
9Ndipo nafsi yangu itashangilia katika Mwenyezi Mungu
na kuufurahia wokovu wake.
10Nitapaza sauti yangu nikisema,
“Ni nani aliye kama wewe, Ee Mwenyezi Mungu?
Wewe huwaokoa maskini kutokana na wale waliowazidi nguvu,
unawaokoa maskini na wahitaji kutokana na wanaowanyang’anya!”
11Mashahidi wakatili wanainuka,
wananiuliza mambo nisiyoyajua.
12Wananilipa baya kwa jema
na kuiacha nafsi yangu ukiwa.
13Lakini walipokuwa wagonjwa, nilivaa gunia
na nikajinyenyekeza kwa kufunga.
Maombi yangu yaliponirudia bila kujibiwa,
14niliendelea kuomboleza
kama vile wao ni rafiki au ndugu.
Niliinamisha kichwa chini kwa huzuni
kama ninayemwombolezea mama yangu.
15Lakini nilipojikwaa,
walikusanyika kwa shangwe;
washambuliaji walijikusanya dhidi yangu
bila mimi kujua.
Walinisingizia pasipo kukoma.
16Kama watu wasiomcha Mungu, wamenidhihaki,
wamenisagia meno.
17Ee Bwana, utatazama hadi lini?
Niokoe maisha yangu na maangamizi yao,
okoa uhai wangu wa thamani
kutokana na simba hawa.
18Nami nitakushukuru mbele ya kusanyiko kubwa,
nitakusifu katikati ya watu wengi.
19Usiwaache wale wanaonisimanga,
wale ambao ni adui zangu bila sababu;
usiwaache wale ambao ni adui zangu bila sababu
wakonyeze jicho kwa hila.
20Hawazungumzi kwa amani,
bali wanatunga mashtaka ya uongo
dhidi ya wale wanaoishi
kwa utulivu katika nchi.
21Hunifumbulia vinywa vyao wakisema, “Aha! Aha!
Kwa macho yetu wenyewe tumeliona.”
22Ee Mwenyezi Mungu, umeona hili, usiwe kimya.
Usiwe mbali nami, Ee Bwana.
23Amka, inuka unitetee!
Unipiganie Mungu wangu na Bwana wangu.
24Nihukumu kwa haki yako, Ee Mwenyezi Mungu, Mungu wangu,
sawasawa na haki yako;
usiwaache wakusimange.
25Usiwaache wafikiri, “Aha, hili ndilo tulilotaka!”
Au waseme, “Tumemmeza.”
26Wote wanaofurahia dhiki yangu
waaibishwe na wachanganyikiwe;
hao wanaojiinua dhidi yangu
wavikwe aibu na dharau.
27Wale wanaofurahia hukumu yangu ya haki
wapige kelele za shangwe na furaha;
hebu waseme siku zote, “Mwenyezi Mungu atukuzwe,
ambaye amefurahia mafanikio ya mtumishi wake.”
28Ulimi wangu utanena haki yako
na sifa zako mchana kutwa.
Iliyochaguliwa sasa
Zaburi 35: NENO
Kuonyesha
Shirikisha
Nakili
Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia
Neno: Maandiko Matakatifu™ NMM™
Hakimiliki © 2018, 2024 na Biblica, Inc.
Imetumiwa kwa ruhusa.
Haki zote zimehifadhiwa duniani kote.
Kiswahili Contemporary Scriptures™
Copyright © 2018, 2024 by Biblica, Inc.
Used with permission. All rights reserved worldwide.