Isaya 17
17
Neno dhidi ya Dameski
1Neno la unabii kuhusu Dameski:
“Tazama, Dameski haitakuwa tena mji
bali itakuwa lundo la magofu.
2Miji ya Aroeri itaachwa
na itaachiwa mifugo ambayo italala huko,
bila yeyote wa kuyaogopesha.
3Mji wenye ngome utatoweka kutoka Efraimu,
nao uweza wa ufalme kutoka Dameski;
mabaki ya Aramu yatakuwa
kama utukufu wa Waisraeli,”
asema Mwenyezi Mungu, Mungu wa majeshi ya mbinguni.
4“Katika siku ile utukufu wa Yakobo utafifia,
unono wa mwili wake utadhoofika.
5Itakuwa kama mvunaji akusanyavyo nafaka
na kuvuna nafaka kwa mikono yake,
kama wakati mtu aokotapo masazo ya masuke
katika Bonde la Warefai.
6Hata hivyo baadhi ya masazo yatabaki,
kama vile mti wa mzeituni unavyopigwa,
kukiachwa zeituni mbili au tatu juu ya matawi kileleni,
nne au tano katika matawi yanayozaa sana,”
asema Mwenyezi Mungu, Mungu wa Israeli.
7Katika siku ile watu watamwangalia Muumba wao,
na kuelekeza macho yao kwa yule Aliye Mtakatifu wa Israeli.
8Hawataziangalia tena madhabahu,
kazi za mikono yao,
nao hawataheshimu nguzo za Ashera,
na madhabahu za kufukizia uvumba zilizofanywa kwa mikono yao.
9Katika siku ile miji yao iliyo imara, ambayo waliihama kwa sababu ya Waisraeli, itakuwa kama mahali palipoachwa pa vichaka na magugu. Nayo yote itakuwa ukiwa.
10Mmemsahau Mungu Mwokozi wenu,
hamkumkumbuka Mwamba aliye ngome yenu.
Kwa hiyo, hata ingawa mlipandikiza mimea iliyo mizuri sana
na kuotesha mizabibu ya kigeni,
11hata kama siku ile unapoipandikiza, unaifanya iote
na asubuhi ile ile unayoipanda, unaifanya ichipue,
hata hivyo mavuno yatakuwa kama si kitu
katika siku ile ya ugonjwa na maumivu yasiyoponyeka.
12Ole! Ghadhabu ya mataifa mengi:
wanaghadhibika kama bahari iliyochafuka!
Ole! Makelele ya mataifa wanaovuma:
wanavuma kama ngurumo za maji mengi!
13Ingawa mataifa yanavuma kama ngurumo za maji yanayofanya mawimbi,
wakati anayakemea yanakimbia mbali,
yanafukuzwa mbele ya upepo kama makapi juu ya milima,
kama jani likivingirishwa na dhoruba.
14Wakati wa jioni, hofu ya ghafula!
Kabla ya asubuhi, wametoweka!
Hili ndilo fungu la wale wanaotupora,
fungu la wale wanaotunyang’anya mali yetu.
Iliyochaguliwa sasa
Isaya 17: NENO
Kuonyesha
Shirikisha
Nakili

Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia
Neno: Maandiko Matakatifu™ NMM™
Hakimiliki © 2018, 2024 na Biblica, Inc.
Imetumiwa kwa ruhusa.
Haki zote zimehifadhiwa duniani kote.
Kiswahili Contemporary Scriptures™
Copyright © 2018, 2024 by Biblica, Inc.
Used with permission. All rights reserved worldwide.