Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

1 Nyakati 17:1-15

1 Nyakati 17:1-15 NEN

Baada ya Daudi kuingia rasmi katika jumba lake la kifalme, akamwambia nabii Nathani, “Hebu tazama, mimi ninakaa kwenye nyumba nzuri iliyojengwa kwa mierezi, wakati Sanduku la Agano la BWANA liko ndani ya hema.” Nathani akamjibu Daudi, “Lolote ulilo nalo moyoni mwako litende, kwa maana Mungu yu pamoja nawe.” Usiku ule neno la Mungu likamjia Nathani, kusema: “Nenda ukamwambie mtumishi wangu Daudi, ‘Hili ndilo asemalo BWANA: Wewe hutanijengea mimi nyumba ili nikae humo. Mimi sijakaa ndani ya nyumba tangu siku ile niliyowatoa Israeli kutoka Misri mpaka leo. Nimehama kutoka hema moja hadi jingine na kutoka mahali pamoja hadi pengine. Je, popote nilipokwenda pamoja na Waisraeli wote, wakati wowote nilimwambia kiongozi yeyote niliyemwagiza kuwachunga watu wangu, kwa nini hujanijengea nyumba ya mierezi?’  “Sasa basi, mwambie mtumishi wangu Daudi, ‘Hili ndilo asemalo BWANA Mwenye Nguvu Zote: Nilikuchukua machungani na kutoka kuandama kondoo ili uwatawale watu wangu Israeli. Nimekuwa pamoja nawe popote ulipokwenda, nami nimekuondolea mbali adui zako wote mbele yako. Basi nitalifanya jina lako kuwa kuu kama majina ya watu walio wakuu sana duniani. Nami nitawapatia watu wangu Israeli mahali na nitawapa ili wawe na mahali pao wenyewe pa kuishi na wasisumbuliwe tena. Watu waovu hawatawaonea tena, kama walivyofanya mwanzoni, na ambavyo wamefanya siku zote tangu nilipowachagua viongozi kwa ajili ya watu wangu Israeli. Pia nitawatiisha adui zenu wote. “ ‘Pamoja na hayo ninakuambia kwamba BWANA atakujengea nyumba: Wakati wako utakapokuwa umekwisha, nawe ukawa umekwenda kukaa na baba zako, nitamwinua mzao wako aingie mahali pako kuwa mfalme, mmoja wa wana wako mwenyewe, nami nitaufanya imara ufalme wake. Yeye ndiye atakayejenga nyumba kwa ajili yangu, nami nitakifanya imara kiti cha ufalme wake milele. Mimi nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwanangu. Kamwe sitaondoa upendo wangu kwake, kama nilivyouondoa kwa yeye aliyekutangulia. Nitamweka juu ya nyumba yangu na ufalme wangu milele; kiti chake cha enzi nitakifanya imara milele.’ ” Nathani akamwarifu Daudi maneno yote ya maono haya.