Mwanzo 39
39
Muke wa Potifari na Yosefu
1Basi, Yosefu aliposhushwa kwenda mpaka Misri, Mumisri mumoja anayeitwa Potifari ambaye alikuwa jemadari wa mufalme wa Misri na mukubwa wa waaskari walinzi, akamununua kutoka kwa Waisimaeli waliomuleta Misri. 2Yawe alikuwa pamoja na Yosefu, akamufanikisha sana. Yosefu akakuwa anakaa katika nyumba ya bwana wake Mumisri. 3Yule bwana wake akatambua kwamba Yawe alikuwa pamoja na Yosefu, na kwamba ndiye aliyefanikisha mambo yote Yosefu aliyofanya. 4Basi, Yosefu akapata kukubaliwa mbele ya Potifari, hata akakuwa mutumishi wake wa pekee. Akamufanya musimamizi wa nyumba yake na mwangalizi wa mali yake yote. 5Tokea wakati Potifari alipomufanya Yosefu kuwa musimamizi wa nyumba yake na mwangalizi wa mali yake, Yawe akabariki nyumba ya yule Mumisri kwa ajili ya Yosefu. Baraka za Yawe zikakuwa juu ya kila kitu alichokuwa nacho, ndani ya nyumba na katika shamba. 6Kwa sababu hiyo Potifari alimupa Yosefu mamlaka juu ya mambo yake yote, naye Potifari akaacha kushugulika na chochote isipokuwa tu chakula chake mwenyewe.
Yosefu alikuwa kijana muzuri na wa kupendeza. 7Basi, nyuma ya muda fulani, muke wa Potifari akamutamani Yosefu na kumwambia: “Lala na mimi”.
8Lakini Yosefu akakataa na kumwambia yule muke wa bwana wake: “Sikiliza! Bwana wangu amenipa mamlaka juu ya kila kitu hapa ndani ya nyumba na hajishugulishi na kitu chochote tena. 9Hapa ndani ya nyumba yeye hana madaraka kuliko mimi. Yeye hakunikataza kushika chochote isipokuwa wewe tu kwa sababu wewe ni muke wake. Nitaweza namna gani basi kufanya uovu mubaya kama ule na kumukosea Mungu?”
10Yule mwanamuke akaendelea kumushawishi Yosefu siku kwa siku, lakini Yosefu hakumusikiliza wala kukubali kulala naye.
11Siku moja, Yosefu akaingia ndani ya nyumba kufanya kazi yake kama kawaida, na watumishi wengine hawakukuwa ndani ya nyumba. 12Basi, muke wa Potifari akamushika nguo yake na kumwambia: “Lala na mimi!”
Lakini Yosefu akamwachia nguo yake katika mikono yake, akakimbilia inje. 13Kwa hiyo, yule mwanamuke alipoona kwamba Yosefu ameacha nguo yake katika mikono yake na kukimbilia inje, 14akaita watumishi wa nyumba yake na kuwaambia: “Huyu Mwebrania tuliyeletewa anatuzarau. Alikuja kwangu akitaka kunishika kwa nguvu, lakini nikapiga kelele. 15Aliposikia ninapiga kelele, akaacha nguo yake, akakimbilia inje!”
16Basi, yule mwanamuke akaweka nguo ile mpaka wakati mume wake aliporudi ndani ya nyumba. 17Akamwelezea jambo lile akisema: “Huyu mutumishi Mwebrania uliyemuleta kwetu alinifikia kwa kunizarau. 18Lakini mara tu nilipopiga kelele, akaacha nguo yake na kukimbilia inje.”
19Basi, bwana wa Yosefu aliposikia maneno ya muke wake, kwamba ndivyo mutumishi wake alivyomutendea, akawaka hasira. 20Akamutwaa Yosefu na kumutia katika kifungo, pahali wafungwa wa mufalme walipokuwa. Lakini hata mule katika kifungo, 21Yawe alikuwa pamoja na Yosefu na kumutendea mema, hata kumufanya apate kukubaliwa mbele ya mukubwa wa kifungo. 22Hivyo mukubwa wa kifungo akamuweka Yosefu akuwe mukubwa wa wafungwa wote mule katika kifungo. Kila kitu kilichofanyika mule kilifanywa kwa mamlaka yake. 23Yule mukubwa wa kifungo hakujishugulisha tena na kitu chochote Yosefu alichopewa kwa maana Yawe alikuwa pamoja na Yosefu na kufanikisha kila kitu alichofanya.
Currently Selected:
Mwanzo 39: SWC02
Highlight
Share
Copy

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.