Esta 4:12-17
Esta 4:12-17 Biblia Habari Njema (BHN)
Mordekai alipopata ujumbe wa Esta, mara alimpelekea onyo hili: “Usidhani kwamba kwa kuwa upo ikulu wewe u salama zaidi kuliko Myahudi mwingine yeyote yule. Ukikaa kimya wakati kama huu, msaada utawajia Wayahudi kutoka mahali pengine, nao wataokolewa; lakini wewe utakufa, na jamaa ya baba yako itaangamia. Ni nani ajuaye pengine umefanywa malkia kwa ajili ya wakati kama huu!” Esta alimpelekea Mordekai jibu hili: “Nenda ukawakusanye pamoja Wayahudi wote waliopo mjini Susa. Fungeni, msile wala msinywe kwa siku tatu, usiku na mchana, kwa ajili yangu. Na mimi na watumwa wa kike wangu tutafanya vivyo hivyo. Kisha, nitamwendea mfalme, ingawa ni kinyume cha sheria. Kama ni kuuawa, na niuawe.” Basi, Mordekai akaenda zake na kufanya kama Esta alivyomwambia.
Esta 4:12-17 Swahili Revised Union Version (SRUV)
Basi wakamwambia Mordekai maneno ya Esta. Naye Mordekai akawaagiza wampelekee Esta jibu la kusema, Wewe usijidhanie kuwa wewe utaokoka nyumbani mwa mfalme, zaidi ya Wayahudi wote. Kwa maana wewe ukinyamaza kabisa wakati huu, ndipo kutakapowatokea Wayahudi msaada na wokovu kwa njia nyingine; ila wewe utaangamia pamoja na mlango wote wa baba yako; lakini ni nani ajuaye kama wewe hukuujia ufalme kwa ajili ya wakati kama huu? Basi Esta akawatuma ili wamjibu Mordekai, Nenda ukawakusanye Wayahudi wote waliopo hapa Susa, mkafunge kwa ajili yangu; msile wala kunywa muda wa siku tatu, usiku wala mchana, nami na wajakazi wangu tutafunga vile vile; kisha nitaingia kwa mfalme, kinyume cha sheria; nami nikiangamia, na niangamie. Basi Mordekai akaenda zake, akafanya yote kama vile Esta alivyomwagiza.
Esta 4:12-17 Maandiko Matakatifu ya Mungu Yaitwayo Biblia (SUV)
Basi wakamwambia Mordekai maneno ya Esta. Naye Mordekai akawaagiza wampelekee Esta jibu la kusema, Wewe usijidhanie kuwa wewe utaokoka nyumbani mwa mfalme, zaidi ya Wayahudi wote. Kwa maana wewe ukinyamaza kabisa wakati huu, ndipo kutakapowatokea Wayahudi msaada na wokovu kwa njia nyingine; ila wewe utaangamia pamoja na mlango wote wa baba yako; walakini ni nani ajuaye kama wewe hukuujia ufalme kwa ajili ya wakati kama huo? Basi Esta akawatuma ili wamjibu Mordekai, Uende ukawakusanye Wayahudi wote waliopo hapa Shushani, mkafunge kwa ajili yangu; msile wala kunywa muda wa siku tatu, usiku wala mchana, nami na wajakazi wangu tutafunga vile vile; kisha nitaingia kwa mfalme, kinyume cha sheria; nami nikiangamia, na niangamie. Basi Mordekai akaenda zake, akafanya yote kama vile Esta alivyomwagiza.
Esta 4:12-17 Neno: Bibilia Takatifu (NEN)
Wakati Mordekai aliarifiwa maneno ya Esta, Mordekai alirudisha jibu hili: “Usifikiri kwamba kwa sababu uko katika nyumba ya mfalme wewe pekee katika Wayahudi wote utapona. Kwa kuwa kama utakaa kimya wakati huu, msaada na ukombozi kwa Wayahudi utatoka mahali pengine, lakini wewe na jamaa ya baba yako mtaangamia. Nani ajuaye kwamba hukuja kwenye nafasi ya mamlaka kwa ajili ya wakati kama huu?” Kisha Esta alituma jibu hili kwa Mordekai: “Nenda, kusanya pamoja Wayahudi wote walioko Shushani, nanyi mfunge kwa ajili yangu. Msile wala kunywa kwa siku tatu, usiku na mchana. Mimi na wajakazi wangu tutafunga kama mnavyofanya. Baada ya kufanyika hili, nitakwenda kwa mfalme, hata ingawa ni kinyume cha sheria. Ikiwa ni kuangamia na niangamie.” Kwa hiyo Mordekai alikwenda zake na kutekeleza maagizo yote ya Esta.