2 Mambo ya Nyakati 19:4-11
2 Mambo ya Nyakati 19:4-11 Biblia Habari Njema (BHN)
Mfalme Yehoshafati alikaa Yerusalemu, lakini hata hivyo, mara kwa mara aliwatembelea watu wa Beer-sheba kusini, mpaka milima ya Efraimu, upande wa kaskazini. Alifanya hivyo ili kuwavutia watu wamrudie Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zao. Aliteua waamuzi katika miji yote ya Yuda yenye ngome, akawaambia, “Muwe waangalifu sana wakati mnapoamua, kwa maana hukumu mtoayo hamwitoi kwa amri ya binadamu, bali kwa amri itokayo kwa Mwenyezi-Mungu, naye yu pamoja nanyi mnapotoa uamuzi. Basi, sasa mwogopeni Mwenyezi-Mungu, muwe waangalifu katika kila jambo mtakalotenda kwa sababu Mwenyezi-Mungu wetu hatavumilia upotoshaji wa haki, wala upendeleo wala ulaji rushwa.” Mjini Yerusalemu, Yehoshafati aliteua Walawi kadhaa, waamuzi na baadhi ya wakuu wa jamaa za Waisraeli wawe waamuzi wa magomvi yahusuyo uvunjaji wa sheria za Mwenyezi-Mungu, au ugomvi baina ya wakazi wa mji. Akawaamuru akisema; “Tekelezeni wajibu wenu mkimwogopa Mwenyezi-Mungu, kwa uaminifu na kwa moyo wote. Kila mara ndugu zenu kutoka katika mji wowote ule wanapowaletea shtaka lolote kuhusu uuaji, uvunjaji wa sheria, amri, kanuni au maagizo, washaurini vema ili wasije wakamkosea Mwenyezi-Mungu. Msipofanya hivyo, nyinyi pamoja na ndugu zenu mtapatwa na ghadhabu ya Mwenyezi-Mungu. Lakini mkiutekeleza wajibu wenu, hamtakuwa na hatia. Amaria, kuhani mkuu, ndiye atakayesimamia mambo yote yanayomhusu Mwenyezi-Mungu, naye Zebadia mwana wa Ishmaeli, gavana wa Yuda atasimamia mambo yote ya utawala, na Walawi watakuwa maofisa. Jipeni moyo muyatekeleze masharti haya, naye Mwenyezi-Mungu awe pamoja nao walio wema.”
2 Mambo ya Nyakati 19:4-11 Swahili Revised Union Version (SRUV)
Na Yehoshafati akakaa Yerusalemu; akatoka tena kwenda kati ya watu toka Beer-sheba mpaka milima ya Efraimu, akawarudisha kwa BWANA, Mungu wa baba zao. Akateua waamuzi katika nchi, katikati ya miji yote yenye maboma ya Yuda, mji kwa mji; akawaambia hao waamuzi, Angalieni myafanyayo; kwa kuwa hammfanyii mwanadamu hukumu, ila BWANA; naye yupo pamoja nanyi katika neno la hukumu. Basi sasa hofu ya BWANA na iwe juu yenu; aiweni waangalifu katika jambo mtendalo, kwa maana kwa BWANA, Mungu wetu hakuna upotoshaji wala kupendelea nafsi za watu au kupokea rushwa. Tena katika Yerusalemu Yehoshafati akateua baadhi ya Walawi na makuhani, na wakuu wa jamaa za Waisraeli wawe waamuzi kwa hukumu za BWANA na kesi kati yao. Nao wakarudi Yerusalemu. Akawaagiza, akasema, Ndivyo mtakavyotenda kwa hofu ya BWANA, kwa uaminifu, na kwa moyo wote. Na kila mara watakapowaletea shitaka toka ndugu zenu wakaao mijini mwao, kuhusu uuaji, uvunjaji wa sheria na amri, kanuni au maagizo, mtawaonya, wasiingie hatiani mbele za BWANA, mkajiliwa na ghadhabu ninyi na ndugu zenu; fanyeni haya wala hamtakuwa na hatia. Tena angalieni, Amaria, kuhani mkuu, yuko juu yenu kwa maneno yote ya BWANA; naye Zebadia, mwana wa Ishmaeli, jemadari wa nyumba ya Yuda, kwa mambo yote ya mfalme; Walawi nao watakuwa wasimamizi mbele yenu. Jitieni nguvu, mtende, naye BWANA awe pamoja nao walio wema.
2 Mambo ya Nyakati 19:4-11 Maandiko Matakatifu ya Mungu Yaitwayo Biblia (SUV)
Na Yehoshafati akakaa Yerusalemu; akatoka tena kwenda kati ya watu toka Beer-sheba mpaka milima ya Efraimu, akawarudisha kwa BWANA, Mungu wa baba zao. Akasimamisha makadhi katika nchi, katikati ya miji yote yenye maboma ya Yuda, mji kwa mji; akawaambia hao makadhi, Angalieni myafanyayo; kwa kuwa hammfanyii mwanadamu hukumu, ila BWANA; naye yupo pamoja nanyi katika neno la hukumu. Basi sasa hofu ya BWANA na iwe juu yenu; angalieni mkaifanye; kwa maana kwa BWANA, Mungu wetu, hapana uovu, wala kujali nafsi za watu, wala kupokea zawadi. Tena katika Yerusalemu Yehoshafati akasimamisha wa Walawi na makuhani, na wakuu wa mbari za mababa wa Israeli wawe kwa hukumu ya BWANA, na kwa mateto. Nao wakarudi Yerusalemu. Akawaagiza, akasema, Ndivyo mtakavyotenda kwa hofu ya BWANA, kwa uaminifu, na kwa moyo kamili. Na kila mara watakapowajia na teto ndugu zenu wakaao mijini mwao, kati ya damu na damu, kati ya torati na amri, sheria na hukumu, mtawaonya, wasiingie hatiani mbele za BWANA, mkajiliwa na ghadhabu ninyi na ndugu zenu; fanyeni haya wala hamtakuwa na hatia. Tena angalieni, Amaria, kuhani mkuu, yu juu yenu kwa maneno yote ya BWANA; naye Zebadia, mwana wa Ishmaeli, jemadari wa nyumba ya Yuda, kwa maneno yote ya mfalme; Walawi nao watakuwa wasimamizi mbele yenu. Jitieni nguvu, mtende, naye BWANA awe pamoja nao walio wema.
2 Mambo ya Nyakati 19:4-11 Neno: Bibilia Takatifu (NEN)
Yehoshafati aliishi huko Yerusalemu, naye akatoka akaenda tena miongoni mwa watu, kuanzia Beer-Sheba hadi nchi ya vilima ya Efraimu na kuwageuza wakamrudia BWANA, Mungu wa baba zao. Akawaweka waamuzi katika nchi, kwenye miji yote ya Yuda yenye maboma. Akawaambia, “Angalieni kwa makini yale mtendayo, kwa kuwa hamkuhukumu kwa ajili ya mwanadamu bali kwa ajili ya BWANA ambaye yu pamoja nanyi kila mtoapo hukumu. Basi sasa hofu ya BWANA na iwe juu yenu. Hukumuni kwa uangalifu, kwa kuwa kwa BWANA Mungu wetu hakuna jambo lisilo la haki, upendeleo, wala rushwa.” Pia huko Yerusalemu, Yehoshafati akaweka baadhi ya Walawi, makuhani na viongozi wa jamaa za Waisraeli ili kutoa hukumu kwa ajili ya BWANA na kuamua magomvi. Nao waliishi huko Yerusalemu. Akawapa maagizo haya: “Ni lazima mtumike kwa uaminifu na kwa moyo wote katika kicho cha BWANA. Katika kila shauri lifikalo mbele yenu kutoka kwa ndugu zenu wale waishio katika miji, ikiwa ni la umwagaji wa damu au mambo mengine yahusuyo sheria, amri, hukumu au maagizo, inawapasa ninyi kuwaonya kwamba wasiingie katika hatia dhidi ya BWANA, la sivyo ghadhabu yake itakuja juu yenu na ndugu zenu. Tendeni hivyo, nanyi hamtatenda dhambi. “Amaria kuhani mkuu atakuwa juu yenu katika jambo lolote linalomhusu BWANA naye Zebadia mwana wa Ishmaeli, kiongozi wa kabila la Yuda, atakuwa juu yenu kwa jambo lolote linalomhusu mfalme, nao Walawi watatumika kama maafisa mbele yenu. Tendeni kwa ujasiri, naye BWANA atakuwa pamoja na wale watendao vyema.”