Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Yobu 8

8
1Ndipo Bildadi, Mshuhi, akamjibu Yobu:
2“Utasema mambo haya mpaka lini?
Mpaka lini maneno yako yatakuwa matupu kama upepo?
3Kwani, wadhani Mungu hupotosha haki?
Au, je, Mungu Mwenye Nguvu hupotosha ukweli?
4Kama watoto wako wamemkosea Mungu,
yeye amewalipiza matokeo ya uhalifu wao.
5Kama utamtafuta Mungu
ukamsihi huyo Mungu mwenye nguvu,
6kama wewe u safi moyoni na mnyofu,
kweli Mungu atakuja kukusaidia,
na kukujalia makao unayostahili.
7Na ingawa ulianza kuishi kwa unyonge
maisha yako ya baadaye yatakuwa ya fahari zaidi.
8Jifunze tafadhali kwa wale waliotutangulia,
zingatia mambo waliyogundua hao wazee.
9Sisi ni watu wa juzijuzi tu, hatujui kitu;
siku zetu duniani ni kivuli kipitacho.
10Lakini wao watakufunza na kukuambia,
mambo waliyopata kuyatoa katika maarifa yao:
11Mafunjo huota tu penye majimaji,
matete hustawi mahali palipo na maji.
12Hata kama yamechanua na bila kukatwa,
yakikosa maji hunyauka kabla ya mimea mingine.
13Ndivyo walivyo wote wanaomsahau Mungu.
Tumaini la wasiomwamini Mungu litapotea.
14Tegemeo lao huvunjikavunjika,#8:14 huvunjikavunjika: Kadiri ya wengine neno la Kiebrania ambalo hutumiwa tu hapa.
tumaini lao ni utando wa buibui.
15Wanaegemea nyumba yao lakini haitasimama,
huishikilia lakini haidumu.
16Jua litokapo yeye hustawi;
hueneza matawi yake bustanini mwake.
17Mizizi yake hujisokotasokota kwenye mawe
naye aenda kuchunguza ndani ya mwamba.#8:17 naye … mwamba: Maana katika Kiebrania si dhahiri.
18Lakini akiangamizwa kutoka makao yake,
hayo yatamkana yakisema: ‘Sijapata kukuona.’
19Tazama, huo ndio mwisho wa furaha ya mtu huyo,
na mahali pao patachipua wengine.
20“Tazama! Mungu hatamkataa mtu asiye na hatia,
wala kuwasaidia waovu.
21Ila atakijaza kinywa chako kicheko,
na midomo yako sauti ya furaha.
22Wale wakuchukiao wataingiwa na aibu,
makao ya waovu yatatoweka kabisa.”

Iliyochaguliwa sasa

Yobu 8: BHN

Kuonyesha

Shirikisha

Nakili

None

Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia