Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Waamuzi 5

5
Wimbo wa Debora
1Siku hiyo, Debora na Baraki, mwana wa Abinoamu, wakaimba wimbo huu:
2“Viongozi walijitokeza kuongoza Israeli,
watu walijitolea kwa hiari yao.
Mshukuruni Mwenyezi-Mungu!
3“Sikilizeni, enyi wafalme!
Tegeni sikio, enyi wakuu!
Nitamwimbia Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli.
4“Ee Mwenyezi-Mungu, ulipotoka huko Seiri,
ulipoteremka mlimani Edomu,
nchi ilitetemeka,
mbingu zilidondosha maji,
naam, mawingu yakaiangusha mvua.
5Milima ilitikisika mbele yako Mwenyezi-Mungu,
naam, mlima Sinai mbele yako Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli.
6“Katika siku za Shamgari, mwana wa Anathi,
katika wakati wa Yaeli,
misafara ilikoma kupita nchini,
wasafiri walipitia vichochoroni.
7Wakulima walikoma kuwako,
walikoma kuwako katika Israeli,
mpaka nilipotokea mimi Debora,
mimi niliye kama mama wa Israeli.
8Walijichagulia miungu mipya,
kukawa na vita katika nchi.
Lakini hakukupatikana mwenye upanga au ngao
kati ya watu 40,000 wa Israeli.
9Nawapa heshima makamanda wa Israeli
waliojitoa kwa hiari yao kati ya watu.
Mshukuruni Mwenyezi-Mungu!
10“Tangazeni, enyi wapandapunda weupe,
enyi mnaokalia mazulia ya fahari,
nyinyi mnaotembea njiani, tangazeni jambo hilo.
11Imbeni kupita wanamuziki kwenye visima vya maji,
tangazeni ushindi wa Mwenyezi-Mungu,
ushindi kwa wakulima wake katika Israeli.
Ndipo watu wa Mwenyezi-Mungu waliposhuka malangoni.
12“Amka, amka, Debora!
Amka! Amka uimbe wimbo!
Amka, Baraki mwana wa Abinoamu,
uwachukue mateka wako.
13Mashujaa waliobaki waliteremka,
watu wa Mwenyezi-Mungu walikwenda kumpigania
dhidi ya wenye nguvu.
14Kutoka Efraimu waliteremka bondeni,#5:14 bondeni: Makala ya Kiebrania; katika Maaleki.
wakafuata ndugu zao watu wa Benyamini;
kutoka Makiri walishuka makamanda,
kutoka Zebuluni maofisa wakuu.
15Wakuu wa Isakari wakafuatana na Debora,
watu wa Isakari waaminifu kwa Baraki;
wakamfuata mbio mpaka bondeni.
Lakini miongoni mwa koo za Reubeni
kulikuwamo kusitasita kwingi.
16Kwa nini walibaki mazizini?
Ili kusikiliza milio ya kondoo?
Miongoni mwa koo za Reubeni
kulikuwamo kusitasita kwingi.
17Kabila la Gileadi lilibaki ngambo ya Yordani.
Kabila la Dani, kwa nini mlibaki merikebuni?
Kabila la Asheri lilitulia huko pwani ya bahari,
lilikaa bandarini mwake.
18Watu wa Zebuluni ni watu
waliohatarisha maisha yao katika kifo.
Hata wa Naftali walikikabili kifo
kwenye miinuko ya mashamba.
19“Huko Taanaki, kando ya chemchemi za Megido,
wafalme walikuja, wakapigana;
wafalme wa Kanaani walipigana,
lakini hawakupata nyara za fedha.
20Nyota kutoka mbinguni zilishiriki vita,
zilifuata njia zao, zilipigana na Sisera.
21Mafuriko ya mto Kishoni yaliwachukua mbali,
naam, mafuriko makali ya mto Kishoni.
Songa mbele kwa nguvu, ee nafsi yangu!
22“Farasi walipita wakipiga shoti;,
walikwenda shoti na kishindo cha kwato zao.
23Malaika wa Mwenyezi-Mungu asema hivi:
‘Uapizeni mji wa Merosi,
waapizeni vikali wakazi wake;
maana hawakuja kumsaidia Mwenyezi-Mungu
hawakumsaidia Mwenyezi-Mungu dhidi ya wenye nguvu’.
24“Abarikiwe kuliko wanawake wote
Yaeli, mke wa Heberi, Mkeni.
Naam, amebarikiwa kuliko wanawake wote
wanaokaa mahemani.
25Sisera alimwomba maji, naye akampa maziwa;
alimletea siagi katika bakuli ya heshima.
26Kwa mkono mmoja alishika kigingi cha hema,
na kwa mkono wake wa kulia nyundo ya fundi;
alimponda Sisera kichwa,
alivunja na kupasuapasua paji lake.
27Sisera aliinama, akaanguka;
alilala kimya miguuni pake.
Hapo alipoinama ndipo alipoanguka, amekufa!
28“Mama yake Sisera alitazama dirishani
alichungulia katika viunzi vyake, akalalamika:
‘Kwa nini gari lake limechelewa?
Mbona vishindo vya magari yake vimechelewa kusikika?’
29Jibu akalipata kwa wanawake wenye hekima:
Akajituliza tena na tena kwa jibu hilo:
30‘Bila shaka wanatafuta na kugawana nyara;
msichana mmoja au wawili kwa kila askari,
vazi la sufu ya rangi kwa ajili ya Sisera.
Vazi la sufu iliyotariziwa,
na mikufu miwili ya nakshi kwa ajili ya shingo yangu!’
31“Ee Mwenyezi-Mungu, waangamie adui zako wote!
Lakini rafiki zako na wawe kama jua,
wakati linapochomoza kwa mwanga mkubwa!”
Nayo nchi ikawa na amani kwa muda wa miaka arubaini.

Iliyochaguliwa sasa

Waamuzi 5: BHN

Kuonyesha

Shirikisha

Nakili

None

Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia

YouVersion hutumia vidakuzi kubinafsisha matumizi yako. Kwa kutumia tovuti yetu, unakubali matumizi yetu ya vidakuzi kama ilivyoelezwa katika Sera yetu ya Faragha