Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Wimbo ulio Bora 8:5-12

Wimbo ulio Bora 8:5-12 SRUV

Ni nani huyu apandaye kutoka nyikani, Akimtegemea mpendwa wake? Nilikuamsha chini ya huo mpera; Huko mama yako alikuonea uchungu, Aliona uchungu aliyekuzaa. Nitie kama mhuri moyoni mwako, Kama mhuri juu ya mkono wako; Kwa maana upendo una nguvu kama mauti, Na wivu ni mkali kama ahera. Mwako wake ni mwako wa moto, Na miali yake ni miali ya Yahu. Maji mengi hayawezi kuuzimisha upendo, Wala mito haiwezi kuuzamisha; Kama mtu angetoa badala ya upendo Mali yote ya nyumbani mwake, Angedharauliwa kabisa. Kwetu sisi tuna dada mdogo, Wala hana matiti; Tumfanyieje dada yetu, Siku atakapoposwa? Kama akiwa tu ukuta, Tumjengee buruji za fedha; Na kama akiwa ni mlango, Tumhifadhi kwa mbao za mierezi. Mimi nilikuwa ukuta, Na matiti yangu kama minara; Ndipo nikawa machoni pake Kama mtu aliyeipata amani. Sulemani alikuwa na shamba la mizabibu huko Baal-hamomi Akawakodisha walinzi hilo shamba lake la mizabibu; Kila mtu atoe vipande elfu moja vya fedha kwa matunda yake. Shamba langu la mizabibu, lililo langu mimi, liko mbele yangu. Basi, Sulemani, wewe uwe na elfu zako, Na hao wayalindao matunda yake wapewe mia mbili.