Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Mithali 31:10-31

Mithali 31:10-31 SRUV

Mke mwema, ni nani awezaye kumwona? Maana thamani yake yapita thamani ya marijani. Moyo wa mumewe humwamini, Wala hatakosa kupata mapato. Humtendea mema wala si mabaya, Siku zote za maisha yake. Hutafuta sufu na kitani; Hufanya kazi yake kwa moyo wote. Afanana na merikebu za biashara; Huleta chakula chake kutoka mbali. Tena huamka, kabla usiku haujaisha; Huwapa watu wa nyumbani mwake chakula; Na wajakazi wake sehemu zao. Huangalia shamba, akalinunua; Kwa mapato ya mikono yake hupanda mizabibu. Hujifunga nguvu viunoni kama mshipi; Hutia mikono yake nguvu. Huona kama bidhaa yake ina faida; Taa yake haizimiki usiku. Hutia mikono yake katika kusokota; Na mikono yake huishika pia. Huwakunjulia maskini mikono yake; Naam, huwanyoshea wahitaji mikono yake. Hawahofii theluji watu wa nyumbani mwake; Maana wote wa nyumbani mwake huvikwa nguo nyekundu. Hujifanyia mazulia ya urembo; Mavazi yake ni kitani safi na urujuani. Mume wake hujulikana malangoni; Aketipo pamoja na wazee wa nchi. Hufanya nguo za kitani na kuziuza; Huwapa wafanya biashara mishipi. Nguvu na hadhi ndiyo mavazi yake; Anaucheka wakati ujao. Hufumbua kinywa chake kwa hekima, Na sheria ya wema iko katika ulimi wake. Huangalia sana njia za watu wa nyumbani mwake; Wala hali chakula cha uvivu. Wanawe huondoka na kumwita heri; Mumewe naye humsifu, na kusema, Binti za watu wengi wamefanya mema, Lakini wewe umewapita wote. Upendeleo hudanganya, na uzuri ni ubatili; Bali mwanamke amchaye BWANA, ndiye atakayesifiwa. Mpe mapato ya mikono yake, Na matendo yake yamsifu malangoni.

Soma Mithali 31

Mipango ya Kusoma Bila Malipo na Ibada zinazohusiana na Mithali 31:10-31