Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Nehemia 4:1-23

Nehemia 4:1-23 SRUV

Lakini ikawa, Sanbalati aliposikia ya kwamba tulikuwa tukiujenga ukuta, akaghadhibika, akawa na uchungu sana, akawadhihaki Wayahudi. Akanena mbele ya nduguze na mbele ya jeshi la Samaria, akisema, Wayahudi hawa wanyonge wanafanyaje? Je! Watajitengenezea boma? Watatoa dhabihu? Au watamaliza katika siku moja? Je! Watayafufua mawe katika chungu hizi za kifusi, nayo yameteketezwa kwa moto? Basi Tobia, Mwamoni, alikuwa karibu naye, akasema, Hata hiki wanachokijenga, angepanda mbweha, angeubomoa ukuta wao wa mawe. Sikia, Ee Mungu wetu; maana tunadharauliwa; ukawarudishie mashutumu yao juu ya vichwa vyao, ukawatoe watekwe katika nchi ya uhamisho; wala usiusitiri uovu wao, wala isifutwe dhambi yao, mbele zako; kwa maana wamekukasirisha mbele ya hao wanaojenga. Basi tukaujenga ukuta; nao ukuta wote ukaunganishwa kiasi cha nusu ya kimo chake; maana watu walikuwa na moyo wa kufanya kazi. Lakini ikawa, Sanbalati, Tobia, Waarabu, Waamoni, na Waashdodi, waliposikia ya kuwa kazi ya kuzitengeneza kuta za Yerusalemu inaendelea, na ya kuwa mahali palipobomoka panaanza kuzibwa, basi wakaghadhibika mno; wakafanya shauri wote pamoja kuja kupigana na Yerusalemu, na kufanya machafuko humo. Bali sisi tulimwomba dua Mungu wetu, tena tukaweka walinzi, mchana na usiku, kwa sababu yao, ili kuwapinga. Lakini Yuda wakasema, Nguvu zao wapagazi zimedhoofika, bado kuna vifusi tele; hatuwezi kuujenga ukuta. Nao adui zetu wakasema, Hawatajua wala kuona, hadi tutakapokuja kati yao, na kuwaua, na kuikomesha kazi hiyo. Kisha Wayahudi waliokaa karibu nao, walikuja, wakatuambia mara kumi: Watakuja kutoka kila sehemu wanapokaa kutushambulia. Basi, nikaweka watu, mahali pa chini pa nafasi iliyokuwa nyuma ya ukuta, mahali palipokuwa wazi, kwa kadiri ya jamaa zao, nikawaweka waliojihami na panga zao, na mikuki yao, na pinde zao. Baada ya kuona haya nilisimama nikawaambia wakuu, maofisa, na watu wengine waliobaki, Msiwaogope; mkumbukeni Bwana, aliye mkuu mwenye kuogofya, mkawapiganie ndugu zenu, wana wenu, binti zenu, wake zenu, na nyumba zenu. Kisha ikawa, adui zetu waliposikia ya kuwa tumekwisha kupata habari, na ya kuwa Mungu amelibatilisha shauri lao, ndipo sisi sote tukarudi ukutani, kila mtu kwa kazi yake. Ikawa tokea wakati huo, nusu ya watumishi wangu walitumika katika kazi hiyo, na nusu yao wakaishika mikuki, na ngao, na pinde, na darii; na viongozi walikuwa nyuma ya nyumba yote ya Yuda. Watu wale walioujenga ukuta, na wale waliochukua mizigo, walijitweka wenyewe, kila mtu alifanya kazi kwa mkono mmoja, na kwa mkono wake wa pili alishika silaha yake; nao wajenzi, kila mtu alikuwa na upanga wake, umefungwa ubavuni mwake, ndivyo alivyojenga. Na yeye aliyepiga baragumu alikuwa karibu na mimi. Nikawaambia wakuu, maofisa na watu wengine; Kazi hii ni nyingi, tena kubwa, nasi tumetawanyika juu ya ukuta, kila mtu akiwa mbali na mwenzake; basi mahali popote mtakaposikia sauti ya baragumu, kimbilieni kwetu; Mungu wetu atatupigania. Hivyo tukajitia katika kazi hiyo; na nusu yao waliishika mikuki, tangu alfajiri hadi nyota zikatokea. Kadhalika, wakati ule ule, nikawaambia watu, Kila mtu na akae ndani ya Yerusalemu pamoja na mtumishi wake, wapate kuwa walinzi wetu wakati wa usiku, na kufanya kazi wakati wa mchana. Basi mimi, na ndugu zangu, na watumishi wangu, na walinzi waliofuatana nami, hatukuvua nguo zetu hata mmoja; kila mtu alikwenda kuteka maji akichukua silaha yake.

Soma Nehemia 4

YouVersion hutumia vidakuzi kubinafsisha matumizi yako. Kwa kutumia tovuti yetu, unakubali matumizi yetu ya vidakuzi kama ilivyoelezwa katika Sera yetu ya Faragha