Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Ayubu 7

7
Ayubu: Mateso yangu hayana mwisho
1 # Ayu 14:5,13,14; Zab 39:4; Mhu 3:1,2 Je! Mtu hana huduma ngumu juu ya nchi?
Na siku zake, je! Si kama siku za mwajiriwa?
2Kama mtumishi atamaniye sana kile kivuli,
Kama mwajiriwa anayetazamia mshahara wake;
3 # Zab 39:5; Mhu 1:14 Hivyo basi nami nimepewa miezi ya ubatili iwe fungu langu,
Nami nimeandikiwa mateso usiku hata usiku.
4Hapo nilalapo chini, nasema,
Nitaondoka lini? Lakini usiku huwa mrefu;
Nami nimejawa na kujitupa huku na huku hata kupambazuke.
5 # Ayu 17:14; Zab 38:5-7; Isa 1:6 Mwili wangu unavikwa mabuu na madongoa ya udongo;
Ngozi yangu hufumba, kisha ikatumbuka tena.
6Siku zangu hupita upesi kuliko chombo cha kufumia,
Nazo zapita pasipokuwa na matumaini.
7 # Zab 78:39; Yak 4:14 Kumbuka ya kwamba maisha yangu ni upepo;
Jicho langu halitaona mema tena.
8 # Ayu 20:9 Jicho lake huyo anionaye halitaniangalia tena;
Macho yako yatanielekea, lakini sitakuwapo.
9 # 2 Sam 12:23; Zab 39:13 Kama vile wingu likomavyo na kutoweka,
Ndivyo alivyo huyo ashukaye kuzimuni, hatazuka tena kabisa.
10Hatarudi tena nyumbani kwake,
Wala mahali pake hapatamjua tena.
11 # Zab 39:1,9 Kwa hiyo sitakizuia kinywa changu;
Nitanena kwa mateso ya roho yangu;
Nitalia kwa uchungu wa nafsi yangu.
12Je! Mimi ni bahari, au je! Ni nyangumi?
Hata ukawaweka walinzi juu yangu?
13Hapo nisemapo, kitanda changu kitanituliza moyo,
Malazi yangu yatanipunguzia kuugua kwangu;
14Ndipo unitishapo kwa ndoto,
Na kunitia hofu kwa maono;
15Hata nafsi yangu huchagua kunyongwa,
Na kuchagua kifo kuliko maumivu yangu haya.
16 # Mwa 27:46; Ayu 10:1; Zab 62:9; Mhu 6:11 Ninadhoofika; sitaishi sikuzote;
Usinisumbue, kwani siku zangu ni uvuvio.
17 # Zab 8:4; 144:3; Ebr 2:6 Je! Mtu ni kitu gani, hata ukamtukuza,
Na kumtia moyoni mwako,
18Na kumwangalia kila asubuhi,
Na kumjaribu kila dakika?
19Je! Hata lini hukomi kuniangalia;
Wala kunisumbua hata nimeze mate?
20 # Zab 36:6 Ikiwa nimefanya dhambi, nikufanyieje, Ee mlinda wanadamu?
Mbona umeniweka niwe shabaha yako,
Hata nimekuwa mzigo kwa nafsi yangu?
21Nawe, je! Mbona hunisamehe makosa yangu,
Na kuniondolea maovu yangu?
Kwa kuwa sasa nitalala mavumbini;
Nawe utanitafuta kwa bidii, lakini sitakuwapo.

Iliyochaguliwa sasa

Ayubu 7: SRUV

Kuonyesha

Shirikisha

Nakili

None

Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia