Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Kol UTANGULIZI

UTANGULIZI
Kolosai ni mji mdogo na wa zamani kwenye bonde la mto Laikusi. Ulipakana na Laodikia, yapata kilomita mia moja hamsini kutoka Efeso. Kanisa la Kolosai labda lilianzishwa na Epafra ambaye alikuwa mwenyeji wa Kolosai (1:7; 4:12).
Epafra alimtembelea Paulo kifungoni kule Rumi (tazama Utangulizi kwa Waraka kwa Waefeso) akampasha habari za Kanisa la Kolosai. Hasa habari kwamba kulikuwa kumezuka mafundisho yasiyo sawa: kwa mfano kushikilia sikukuu kubwa kubwa “mwezi mpya au Sabato” (2:16); na pia “elimu… ya bure… mapokeo ya wanadamu…” (2:8); “Msishike, msionje, msiguse” (2:21); “ibada mliyojitungia wenyewe… kunyenyekea, na kuutawala mwili kwa ukali” (2:23), n.k. Mafundisho mengine yalikataa moja kwa moja umungu wa Yesu. Yote, kwa jumla, yalitishia kupotosha au kuvuruga mafundisho ya kweli ya kikristo kule Kolosai.
Paulo aliwaandikia Waraka huu na kusema kuwa mafundisho hayo ni elimu potovu na udanganyifu mtupu (2:8). Akasisitiza hali ya kimungu ya Yesu Kristo, ambaye kwake “unakaa utimilifu wote wa Mungu kwa jinsi ya kimwili” (2:9). Kutokana na mazingira hayo kule Kolosai, kwa kutumia maandishi ya kishairi au utenzi, Paulo anaonesha kwa uhodari wa uandishi mkubwa ukuu wa Kristo juu ya ulimwengu wote na katika kanisa (1:15-20): Kristo ni “kichwa cha mwili, yaani, cha kanisa” (1:18 rejea Efe 1:22-23), “amekuwako kabla ya vitu vyote, na vitu vyote hushikana katika yeye.” (1:17). Kwa njia ya kifo chake mslabani binadamu mwenye dhambi anakombolewa (1:14) na kupatanishwa na kuwekwa katika amani na Mungu (1:20-22).
Katika 2:6–4:6, Paulo anafundisha juu ya thamani kuu ya injili ya neema. Katika Kristo ukamilifu wote wa Mungu upo (2:9) na katika yeye waumini wanakuwa na ukamilifu wao wenyewe (2:10-15) na kutokana na hilo wanapaswa kuachilia kabisa mambo yote ambayo hayapatani na maisha mapya katika kuungana na Kristo (2:13-17,20-22) na kutafuta mambo ya juu ambapo Kristo anaishi, ameketi upande wa kulia wa Mungu (3:1). Maisha haya mapya lazima yarekebishwe kulingana na misingi ya maisha mapya ya binadamu aliuyeumbwa katika Kristo (3:10): maana Kristo ni yote, na katika yote (3:11).

Iliyochaguliwa sasa

Kol UTANGULIZI: SUV

Kuonyesha

Shirikisha

Nakili

None

Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia