Zaburi 68
68
Zaburi 68
Wimbo wa taifa wa shangwe kwa ushindi
Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi. Wimbo.
1Mungu na ainuke, watesi wake watawanyike,
adui zake na wakimbie mbele zake.
2Kama moshi unavyopeperushwa na upepo,
vivyo hivyo uwapeperushe mbali,
kama nta inavyoyeyuka kwenye moto,
vivyo hivyo waovu na waangamie mbele za Mungu.
3Bali wenye haki na wafurahi,
washangilie mbele za Mungu,
wafurahi na kushangilia.
4Mwimbieni Mungu, liimbieni sifa jina lake,
mtukuzeni yeye anayepita juu ya mawingu:
jina lake ni Mwenyezi Mungu,
furahini mbele zake.
5Baba wa yatima, mtetezi wa wajane,
ni Mungu katika makao yake matakatifu.
6Mungu huwaweka wapweke katika jamaa,
huwaongoza wafungwa wakiimba,
bali waasi huishi katika nchi kame.
7Ee Mungu, ulipowatangulia watu wako,
ulipopita nyikani,
8dunia ilitikisika,
mbingu zikanyesha mvua,
mbele za Mungu, Yule wa Sinai,
mbele za Mungu, Mungu wa Israeli.
9Ee Mungu, ulinyesha mvua nyingi
na kuiburudisha ardhi iliyokuwa imechoka.
10Ee Mungu, watu wako waliishi huko,
nawe kwa wingi wa utajiri wako
uliwapa maskini mahitaji yao.
11Bwana analitoa neno,
wanawake wanaolitangaza
neno hilo ni kundi kubwa:
12“Wafalme na majeshi walikimbia upesi,
wanawake waliobaki nyumbani waligawana nyara.
13Hata unapolala kati ya mioto ya kambini,
mabawa ya njiwa wangu yamefunikwa kwa fedha,
manyoya yake kwa dhahabu inayong’aa.”
14Mwenyezi#68:14 Mwenyezi hapa ina maana ya Shaddai kwa Kiebrania. alipowatawanya wafalme katika nchi,
ilikuwa kama theluji iliyoanguka juu ya Mlima Salmoni.
15Milima ya Bashani ni milima iliyotukuka,
milima ya Bashani ina vilele vilivyochongoka.
16Enyi milima yenye vilele vilivyochongoka,
kwa nini mnakazia macho kwa wivu,
katika mlima Mungu anaochagua kutawala,
ambako Mwenyezi Mungu mwenyewe ataishi milele?
17Magari ya vita ya Mungu ni makumi ya maelfu,
na maelfu ya maelfu;
Bwana amekuja kutoka Sinai
hadi katika patakatifu pake.
18Ulipopanda juu, uliteka mateka,
ukapokea vipawa kutoka kwa wanadamu,
hata kutoka kwa wale walioasi,
ili wewe, Ee Bwana Mwenyezi Mungu, upate kuishi huko.
19Ahimidiwe Bwana, Mungu Mwokozi wetu,
ambaye siku kwa siku hutuchukulia mizigo yetu.
20Mungu wetu ni Mungu anayeokoa,
Bwana Mungu Mwenyezi hutuokoa na kifo.
21Hakika Mungu ataponda vichwa vya adui zake,
vichwa vya hao wanaoenda katika njia za dhambi.
22Bwana alisema, “Nitawarudisha kutoka Bashani;
nitawarudisha kutoka vilindi vya bahari,
23ili uweze kuchovya miguu yako katika damu ya adui zako,
huku ndimi za mbwa wako zikiwa na fungu lake.”
24Ee Mungu, maandamano yako yameonekana,
maandamano ya Mungu wangu, Mfalme wangu,
yakielekea patakatifu pake.
25Mbele wako waimbaji, baada yao wapiga vinanda,
pamoja nao wako wanawali wakipiga matari.
26Msifuni Mungu katika kusanyiko kubwa,
msifuni Mwenyezi Mungu katika kusanyiko la Israeli.
27Liko kabila dogo la Benyamini likiwaongoza,
wakifuatwa na kundi kubwa la watawala wa Yuda,
hatimaye watawala wa Zabuloni na Naftali.
28Ee Mungu, amuru uwezo wako,
Ee Mungu tuoneshe nguvu zako,
kama ulivyofanya hapo awali.
29Kwa sababu ya Hekalu lako Yerusalemu
wafalme watakuletea zawadi.
30Mkemee mnyama aliye kwenye matete,
kundi la mafahali kati ya ndama za mataifa.
Na walete minara ya madini ya fedha wakinyenyekea.
Tawanya mataifa yapendayo vita.
31Wajumbe watakuja kutoka Misri;
Kushi atajisalimisha kwa Mungu.
32Mwimbieni Mungu, enyi falme za dunia,
mwimbieni Bwana sifa,
33mwimbieni sifa yeye apandaye mbingu za kale zilizo juu,
yeye angurumaye kwa sauti kuu.
34Tangazeni uwezo wa Mungu,
ambaye fahari yake iko juu ya Israeli,
ambaye uwezo wake uko katika anga.
35Ee Mungu, wewe unatisha katika mahali patakatifu pako,
Mungu wa Israeli huwapa watu wake uwezo na nguvu.
Ahimidiwe Mungu!
Iliyochaguliwa sasa
Zaburi 68: NENO
Kuonyesha
Shirikisha
Nakili
![None](/_next/image?url=https%3A%2F%2Fimageproxy.youversionapi.com%2F58%2Fhttps%3A%2F%2Fweb-assets.youversion.com%2Fapp-icons%2Fsw.png&w=128&q=75)
Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia
Neno: Maandiko Matakatifu™ NMM™
Hakimiliki © 2018, 2024 na Biblica, Inc.
Imetumiwa kwa ruhusa.
Haki zote zimehifadhiwa duniani kote.
Kiswahili Contemporary Scriptures™
Copyright © 2018, 2024 by Biblica, Inc.
Used with permission. All rights reserved worldwide.