Zaburi 38
38
Zaburi 38
Maombi ya mtu anayeteseka
Zaburi ya Daudi. Maombi.
1Ee Mwenyezi Mungu, usinikemee katika hasira yako,
wala kuniadhibu katika ghadhabu yako.
2Kwa kuwa mishale yako imenichoma,
na mkono wako umenipiga.
3Hakuna afya mwilini mwangu
kwa sababu ya ghadhabu yako,
mifupa yangu haina uzima
kwa sababu ya dhambi zangu.
4Maovu yangu yamenifunika
kama mzigo mzito mno.
5Majeraha yangu yameoza na yananuka,
kwa sababu ya upumbavu wa dhambi zangu.
6Nimeinamishwa chini na kushushwa sana,
mchana kutwa nazunguka nikiomboleza.
7Viuno vyangu vimejaa maumivu yaunguzayo,
hakuna afya mwilini mwangu.
8Nimedhoofika na kupondwa kabisa,
nasononeka kwa maumivu makuu ya moyoni.
9Ee Bwana, yote ninayoyaonea shauku
yako wazi mbele zako,
kutamani kwangu sana
hakufichiki mbele zako.
10Moyo wangu unapigapiga,
nguvu zangu zimeniishia;
hata macho yangu yametiwa giza.
11Rafiki na wenzangu wananikwepa
kwa sababu ya majeraha yangu;
majirani wangu wanakaa mbali nami.
12Wale wanaotafuta uhai wangu
wanatega mitego yao,
wale ambao wangetaka kunidhuru
huongea kuhusu maangamizi yangu;
hupanga hila mchana kutwa.
13Mimi ni kama kiziwi, asiyeweza kusikia,
ni kama bubu, asiyeweza kufungua kinywa chake;
14nimekuwa kama mtu asiyesikia,
ambaye kinywa chake hakiwezi kutoa jibu.
15Ee Mwenyezi Mungu, ninakungojea wewe,
Ee Mwenyezi Mungu, Mungu wangu, utajibu.
16Kwa kuwa nilisema, “Usiwaache wafurahie,
wala wajitukuze juu yangu
mguu wangu unapoteleza.”
17Kwa maana ninakaribia kuanguka,
na maumivu yangu yananiandama siku zote.
18Naungama uovu wangu,
ninataabishwa na dhambi yangu.
19Wengi wamekua adui zangu bila sababu;
wale wanaonichukia bure ni wengi.
20Wanaolipa wema wangu kwa maovu
hunisingizia ninapofuata lililo jema.
21Ee Mwenyezi Mungu, usiniache,
usiwe mbali nami, Ee Mungu wangu.
22Ee Bwana Mwokozi wangu,
uje upesi kunisaidia.
Iliyochaguliwa sasa
Zaburi 38: NENO
Kuonyesha
Shirikisha
Nakili

Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia
Neno: Maandiko Matakatifu™ NMM™
Hakimiliki © 2018, 2024 na Biblica, Inc.
Imetumiwa kwa ruhusa.
Haki zote zimehifadhiwa duniani kote.
Kiswahili Contemporary Scriptures™
Copyright © 2018, 2024 by Biblica, Inc.
Used with permission. All rights reserved worldwide.