Zaburi 30
30
Zaburi 30
Maombi ya shukrani
Utenzi wa kuweka wakfu hekalu. Zaburi ya Daudi.
1Nitakutukuza wewe, Ee Mwenyezi Mungu,
kwa kuwa umeniinua kutoka vilindi,
na hukuacha adui zangu
washangilie juu yangu.
2Ee Mwenyezi Mungu, Mungu wangu, nilikuita unisaidie
na wewe umeniponya.
3Ee Mwenyezi Mungu, umenitoa Kuzimu#30:3 Kuzimu kwa Kiebrania ni Sheol, yaani Shimo lisilo na mwisho.,
umeniokoa nisishuke kwenye shimo la mauti.
4Mwimbieni Mwenyezi Mungu, enyi watakatifu wake;
lisifuni jina lake takatifu.
5Kwa maana hasira yake ni ya muda mfupi,
bali upendo wake hudumu siku zote.
Inawezekana kilio kiwepo usiku kucha,
lakini furaha huja asubuhi.
6Nilipofanikiwa nilisema,
“Sitatikiswa kamwe.”
7Ee Mwenyezi Mungu, uliponijalia,
uliuimarisha mlima wangu,
lakini ulipouficha uso wako
nilifadhaika.
8Kwako wewe, Ee Mwenyezi Mungu, niliita,
niliomba rehema kwa Bwana:
9“Kuna faida gani katika kuangamia kwangu,
katika kushuka kwangu shimoni?
Je, mavumbi yatakusifu?
Je, yatatangaza uaminifu wako?
10Ee Mwenyezi Mungu, unisikie na kunihurumia;
Ee Mwenyezi Mungu, uwe msaada wangu.”
11Uligeuza maombolezo yangu kuwa kucheza,
ulinivua gunia ukanivika shangwe,
12ili moyo wangu uweze kukusifu na usikae kimya.
Ee Mwenyezi Mungu, Mungu wangu, nitakushukuru milele.
Iliyochaguliwa sasa
Zaburi 30: NENO
Kuonyesha
Shirikisha
Nakili

Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia
Neno: Maandiko Matakatifu™ NMM™
Hakimiliki © 2018, 2024 na Biblica, Inc.
Imetumiwa kwa ruhusa.
Haki zote zimehifadhiwa duniani kote.
Kiswahili Contemporary Scriptures™
Copyright © 2018, 2024 by Biblica, Inc.
Used with permission. All rights reserved worldwide.