Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Hesabu 9:15-23

Hesabu 9:15-23 NEN

Katika siku hiyo ambayo Maskani, Hema la Ushuhuda, iliposimamishwa, wingu liliifunika. Kuanzia jioni mpaka asubuhi wingu lililokuwa juu ya Maskani lilionekana kama moto. Hivyo ndivyo lilivyoendelea kuwa; wingu liliifunika wakati wa mchana, na usiku lilionekana kama moto. Wakati wowote wingu lilipoinuka kutoka juu ya Hema, nao Waisraeli waliondoka; mahali popote wingu liliposimama, Waisraeli walipiga kambi. Kwa amri ya BWANA Waisraeli waliondoka, na kwa amri yake walipiga kambi. Kwa muda wote wingu liliposimama juu ya Maskani, Waisraeli walibaki wamepiga kambi. Wakati wingu lilipobaki juu ya Maskani kwa muda mrefu, Waisraeli walitii amri ya BWANA nao hawakuondoka. Wakati mwingine wingu lilikuwa juu ya Maskani kwa siku chache tu; kwa amri ya BWANA wangelipiga kambi na kisha kwa amri yake wangeliondoka. Wakati mwingine wingu lilikuwepo kuanzia jioni mpaka asubuhi tu, na lilipoinuka asubuhi, nao waliondoka. Ikiwa ni mchana au usiku, wakati wowote wingu lilipoinuka, waliondoka. Ikiwa wingu lilikaa juu ya Maskani kwa siku mbili au mwezi au mwaka, Waisraeli wangebaki wamepiga kambi na hawakuondoka; lakini lilipoinuka, wangeondoka. Kwa amri ya BWANA walipiga kambi, na kwa amri ya BWANA waliondoka. Walitii amri ya BWANA, kufuatana na agizo lake kupitia Mose.