Isaya 50
50
Dhambi ya Israeli na utii wa mtumishi
1Hili ndilo asemalo Mwenyezi Mungu:
“Iko wapi hati ya talaka ya mama yako
ambayo kwayo niliachana naye?
Au nimewauza ninyi kwa nani
miongoni mwa watu wanaonidai?
Kwa ajili ya dhambi zenu mliuzwa,
kwa sababu ya makosa, mama yenu aliachwa.
2Nilipokuja, kwa nini hapakuwa hata mtu mmoja?
Nilipoita, kwa nini hapakuwa hata mtu mmoja wa kujibu?
Je, mkono wangu ni mfupi mno hata nisiweze kuwakomboa?
Je, mimi sina nguvu za kukuokoa?
Kwa kukemea tu naikausha bahari,
naigeuza mito ya maji kuwa jangwa;
samaki wake wanaoza kwa kukosa maji
na kufa kwa ajili ya kiu.
3Ninalivika anga weusi na kufanya gunia
kuwa kifuniko chake.”
4Bwana Mungu Mwenyezi amenipa ulimi uliofundishwa,
ili kujua neno limtegemezalo aliyechoka.
Huniamsha asubuhi kwa asubuhi,
huamsha sikio langu lisikie kama mtu afundishwaye.
5Bwana Mungu Mwenyezi amezibua masikio yangu,
nami sikuwa mwasi,
wala sikurudi nyuma.
6Niliwapa mgongo wangu wale wanipigao,
mashavu yangu wale wang’oao ndevu zangu;
sikuuficha uso wangu kutokana na fedheha
na kutemewa mate.
7Kwa sababu Bwana Mungu Mwenyezi ananisaidia,
sitatahayarika.
Kwa hiyo nimekaza uso wangu kama gumegume,
nami ninajua sitaaibika.
8Yeye anipatiaye haki yangu yu karibu.
Ni nani basi atakayeleta mashtaka dhidi yangu?
Tukabiliane uso kwa uso!
Mshtaki wangu ni nani?
Ni nani aliye mshtaki wangu?
9Ni Bwana Mungu Mwenyezi anisaidiaye mimi.
Ni nani huyo atakayenihukumu?
Wote watachakaa kama vazi,
nondo watawala wawamalize.
10Ni nani miongoni mwenu amchaye Mwenyezi Mungu,
na kulitii neno la mtumishi wake?
Yeye atembeaye gizani,
yeye asiye na nuru,
na alitumainie jina la Mwenyezi Mungu,
na amtegemee Mungu wake.
11Lakini sasa, ninyi nyote mnaowasha mioto,
na kupeana mienge iwakayo ninyi kwa ninyi,
nendeni, tembeeni katika nuru ya moto wenu
na ya mienge mliyoiwasha.
Hili ndilo mtakalolipokea kutoka mkononi mwangu:
Mtalala chini kwa mateso makali.
Iliyochaguliwa sasa
Isaya 50: NENO
Kuonyesha
Shirikisha
Nakili

Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia
Neno: Maandiko Matakatifu™ NMM™
Hakimiliki © 2018, 2024 na Biblica, Inc.
Imetumiwa kwa ruhusa.
Haki zote zimehifadhiwa duniani kote.
Kiswahili Contemporary Scriptures™
Copyright © 2018, 2024 by Biblica, Inc.
Used with permission. All rights reserved worldwide.