Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Matendo 2:32-41

Matendo 2:32-41 NENO

Mungu alimfufua huyu Isa, na sisi sote ni mashahidi wa jambo hilo. Basi yeye ametukuzwa hadi mkono wa kuume wa Mungu, na amepokea kutoka kwa Baba ahadi ya Roho Mtakatifu wa Mungu, naye amemimina kile mnachoona sasa na kusikia. Kwa kuwa Daudi hakupaa kwenda mbinguni, lakini anasema, “ ‘Bwana alimwambia Bwana wangu: “Keti mkono wangu wa kuume, hadi nitakapowaweka adui zako chini ya miguu yako.”’ “Kwa hiyo Israeli wote na wajue jambo hili kwa uhakika kwamba: Mungu amemfanya huyu Isa, ambaye ninyi mlimsulubisha, kuwa Bwana na Al-Masihi.” Watu waliposikia maneno haya yakawachoma mioyo yao, wakawauliza Petro na wale mitume wengine, “Ndugu zetu tufanye nini?” Petro akawajibu, “Tubuni, mkabatizwe kila mmoja wenu kwa jina la Isa Al-Masihi, ili mpate kusamehewa dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho wa Mungu. Kwa kuwa ahadi hii ni kwa ajili yenu na watoto wenu, na kwa wote walio mbali, na kila mtu ambaye Bwana Mungu wetu atamwita amjie.” Petro akawaonya kwa maneno mengine mengi na kuwasihi akisema, “Jiepusheni na kizazi hiki kilichopotoka.” Wale wote waliopokea ujumbe wa Petro kwa furaha wakabatizwa, na siku ile waliongezeka watu wapatao elfu tatu.