Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

1 Samweli 2:1-10

1 Samweli 2:1-10 NEN

Kisha Hana akaomba na kusema: “Moyo wangu wamshangilia BWANA, katika BWANA pembe yangu imeinuliwa juu. Kinywa changu chajisifu juu ya adui zangu, kwa kuwa naufurahia wokovu wako. “Hakuna yeyote aliye mtakatifu kama BWANA, hakuna mwingine zaidi yako; hakuna Mwamba kama Mungu wetu. “Msiendelee kusema kwa kiburi hivyo wala msiache vinywa vyenu kunena kwa kiburi, kwa kuwa BWANA ndiye Mungu ajuaye, na kwa yeye matendo hupimwa. “Pinde za mashujaa zimevunjika, lakini wale wanaojikwaa wamevikwa nguvu. Wale waliokuwa na chakula tele wamejikodisha wenyewe ili kupata chakula, lakini wale waliokuwa na njaa hawana njaa tena. Mwanamke yule aliyekuwa tasa amezaa watoto saba, lakini yule ambaye alikuwa na wana wengi amedhoofika. “BWANA huua na huleta uhai, hushusha chini mpaka kaburini na hufufua. BWANA humfanya mtu maskini naye hutajirisha, hushusha na hukweza. Humwinua maskini kutoka mavumbini na humwinua mhitaji kutoka lundo la majivu; huwaketisha pamoja na wakuu na kuwafanya warithi kiti cha enzi cha heshima. “Kwa kuwa misingi ya dunia ni ya BWANA; juu yake ameuweka ulimwengu. Yeye atailinda miguu ya watakatifu wake, lakini waovu watanyamazishwa kwenye giza. “Si kwa nguvu mtu hushinda; wale wampingao BWANA wataharibiwa kabisa. Atapiga radi dhidi yao kutoka mbinguni; BWANA ataihukumu miisho ya dunia.