YouVersion Logo
Search Icon

Amosi 5

5
Maombolezo ya Amosi
1Sikilizeni maombolezo yangu juu yenu,
enyi Waisraeli:
2Umeanguka na hutainuka tena
ewe binti Israeli!
Umeachwa pweke nchini mwako,
hamna hata mtu wa kukuinua.
3Maana Bwana Mwenyezi-Mungu asema hivi:
“Watu 1,000 watatoka mjini kwenda kupigana
lakini watarejea 100 tu;
wataondoka watu 100 wa kijiji kimoja
lakini watanusurika watu kumi tu.”
4Mwenyezi-Mungu awaambia hivi Waisraeli:
“Nitafuteni mimi nanyi mtaishi!
5Lakini msinitafute huko Betheli
wala msiende Gilgali
wala msivuke kwenda Beer-sheba.
Maana wakazi wa Gilgali,
hakika watachukuliwa uhamishoni,
na Betheli utaangamizwa!”
6Mtafuteni Mwenyezi-Mungu, nanyi mtaishi!
La sivyo, atawalipukia wazawa wa Yosefu kama moto;
moto utawateketeza wakazi wa Betheli
na hakuna mtu atakayeweza kuuzima.
7Tahadhari enyi mnaogeuza haki kuwa uchungu,
na kuuona uadilifu kuwa kama takataka!
8Huyo aliyezifanya Kilimia na sayari Orioni,
ambaye huligeuza giza nene kuwa mchana,
na mchana kuwa usiku;
yeye ambaye ayaitaye pamoja maji ya bahari
na kuyamwaga juu ya nchi kavu,
Mwenyezi-Mungu ndilo jina lake.
9Yeye ndiye anayewaangamiza wenye nguvu,
na kuziharibu ngome zao.
10Nyinyi huwachukia watetezi wa haki
na wenye kusema ukweli mahakamani.
11Nyinyi mnawakandamiza fukara
na kuwatoza kodi ya ngano kupita kiasi.
Mnajijengea nyumba za mawe ya kuchonga,
lakini nyinyi hamtaishi humo;
mnalima bustani nzuri za mizabibu,
lakini hamtakunywa divai yake.
12Maana mimi najua wingi wa makosa yenu
na ukubwa wa dhambi zenu;
nyinyi mnawatesa watu wema,
mnapokea rushwa
na kuzuia fukara wasipate haki mahakamani.
13Basi, kutakuwa na wakati mbaya
ambao hata mwenye busara atanyamaza.
14Tafuteni kutenda mema na si mabaya,
ili nyinyi mpate kuishi
naye Mwenyezi-Mungu wa majeshi
awe pamoja nanyi kama mnavyosema.
15Chukieni uovu, pendeni wema,
na kudumisha haki mahakamani.
Yamkini Mwenyezi-Mungu wa majeshi atawafadhili watu wa Yosefu waliobaki.
16Basi, Mwenyezi-Mungu, Mungu wa majeshi,
naam, Mwenyezi-Mungu asema:
“Patakuwa na kilio kila mahali mitaani;
watu wataomboleza: ‘Ole! Ole!’
Wakulima wataitwa waje kuomboleza,
na mabingwa wa kuomboleza waje kufanya matanga.
17Patakuwa na kilio katika mashamba yote ya mizabibu;
maana nitapita kati yenu kuwaadhibu.
Nasema mimi Mwenyezi-Mungu.”
Siku ya Mwenyezi-Mungu
18Ole wenu nyinyi mnaoingojea kwa hamu
siku ya Mwenyezi-Mungu!
Kwa nini mnaitaka sana siku hiyo?
Siku hiyo, itakuwa siku ya giza na sio ya mwanga!
19Mambo yatakuwa kama mtu aliyekimbia simba,
halafu akakumbana na dubu!
Au kama mtu anayerudi nyumbani kwake,
akatia mkono ukutani, akaumwa na nyoka.
20Siku ya Mwenyezi-Mungu itakuwa giza, na sio mwanga;
itakuwa huzuni bila uangavu wowote.
21Mwenyezi-Mungu asema hivi:
“Nazichukia na kuzidharau sikukuu zenu;
siifurahii mikutano yenu ya kidini.
22Mjaponitolea sadaka zenu za kuteketezwa na za nafaka,
mimi sitakubali kuzipokea;
na sadaka zenu za amani za wanyama wanono
mimi sitaziangalia kabisa.
23Ondoeni mbele yangu kelele za nyimbo zenu!
Sitaki kusikiliza muziki wa vinubi vyenu!
24Lakini acheni haki itiririke kama maji,
uadilifu uwe kama mto usiokauka.
25“Enyi Waisraeli, wakati ule mlipokuwa kule jangwani kwa miaka arubaini, je, mliniletea tambiko na sadaka hata mara moja? 26Je, wakati huo mlibeba kama sasa vinyago vya mungu wenu Sakuthi mfalme wenu na vinyago vya Kaiwani mungu wenu wa nyota, vitu ambavyo mlijitengenezea wenyewe? 27Kwa hiyo nitawapeleka uhamishoni, mbali kuliko Damasko! Hayo amesema Mwenyezi-Mungu, ambaye jina lake ni Mungu wa Majeshi.

Currently Selected:

Amosi 5: BHN

Highlight

Share

Copy

None

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in