YouVersion Logo
Search Icon

Mwanzo 8

8
Mwisho wa mafuriko ya maji
1Kisha Mungu akamukumbuka Noa na nyama wote wa pori na wa kufugwa waliokuwa pamoja naye ndani ya chombo. Basi, Mungu akavumisha upepo juu ya inchi, maji yakaanza kupunguka. 2Chemichemi za maji ya vilindi na madirisha ya mbinguni yakafungwa. Mvua ikazuiwa, 3maji yakaendelea kupunguka polepole katika inchi. Nyuma ya siku mia moja na makumi tano, maji yakakuwa yamepunguka sana. 4Katika siku ya kumi na saba ya mwezi wa saba, chombo ikatua juu ya milima ya Ararati. 5Maji yakaendelea kupunguka polepole, na siku ya kwanza ya mwezi wa kumi, vilele vya milima vikaonekana.
6Kisha siku makumi ine, Noa akafungua dirisha alilokuwa ametengeneza katika chombo hicho, 7akatuma kibombobombo inje, naye hakurudi, lakini aliruka kule na kule mpaka maji yalipokauka katika inchi. 8Kisha Noa akatuma njiwa apate kuona kama maji yalikuwa yamepunguka juu ya inchi. 9Lakini kwa vile maji yalikuwa yangali yakifunika inchi yote, yule njiwa hakupata pahali pa kutua, akarudilia Noa katika chombo. Noa akanyoosha mukono, akamutwaa na kumurudisha ndani ya chombo. 10Noa akangoja siku zingine saba, kisha akatuma tena yule njiwa. 11Njiwa yule akamurudilia Noa saa za magaribi akiwa na tawi bichi la muzeituni katika midomo yake. Kwa hiyo Noa akajua kwamba maji yalikuwa yamepunguka katika inchi. 12Kisha akangoja siku zingine saba, akatuma tena yule njiwa; mara hii, njiwa hakurudi kabisa.
13Noa alipokuwa na umri wa miaka mia sita na moja, siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, maji yalikuwa yamekauka katika inchi. Noa akafunua kifuniko cha chombo, na alipoangalia, akaona kwamba inchi ilikuwa imekauka. 14Siku ya makumi mbili na saba ya mwezi wa pili, inchi ilikuwa imekauka kabisa.
15Hapo, Mungu akamwambia Noa: 16“Toka katika chombo, wewe pamoja na muke wako, wana wako na wake zao. 17Ondoa vilevile viumbe vyote vyenye uzima vya kila aina vilivyokuwa pamoja nawe, ndege na nyama na kila kiumbe kinachotambaa, vipate kuzaa kwa wingi katika dunia, viongezeke na kuenea kila pahali katika dunia.” 18Basi, Noa akatoka katika chombo pamoja na wana wake na muke wake pamoja na wake za wana wake. 19Wakatoka, kufuatana na jamii zao, nyama wote wa pori, viumbe vyote vinavyotambaa, ndege wote na nyama wote wenye uzima katika dunia.
Noa anamutolea Mungu sadaka
20Noa akamujengea Yawe mazabahu, akatwaa mumoja katika kila aina ya nyama wanaohesabiwa kuwa safi na ndege anayehesabiwa kuwa safi, akamutolea Mungu sadaka za kuteketezwa kwa moto juu ya mazabahu. 21Harufu nzuri ya sadaka hiyo ikamupendeza Yawe, naye akasema ndani ya moyo wake: “Sitailaani tena inchi hata kidogo kwa sababu ya mwanadamu. Ninajua kwamba mawazo yake ni maovu tangu utoto wake. Wala sitaangamiza tena viumbe vyote kama vile nilivyofanya. 22Kwa kadiri inchi itakavyodumu, wakati wa kupanda na kuvuna, wa baridi na joto, wa mvua na kipwa, usiku na muchana, havitakosa kuwa.”

Currently Selected:

Mwanzo 8: SWC02

Highlight

Share

Copy

None

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in