YouVersion Logo
Search Icon

Mwanzo 6

6
Uovu wa watu
1Wakati watu walipoanza kuongezeka katika dunia na kuzaa wabinti, 2wana wa Mungu#6.2 wana wa Mungu: au: wana wa miungu, au: wakaaji wa mbinguni. wakaona kwamba wale wabinti za watu ni wazuri, wakawatwaa wale waliowapendeza kuwa wake zao. 3Kwa hiyo, Yawe akasema: “Roho yangu haitakaa ndani ya wanadamu milele, maana yeye ni wa kufa tu. Basi, hataishi zaidi ya miaka mia moja na makumi mbili.” 4Katika siku zile na hata kisha, kulikuwa majitu katika dunia ambao walikuwa wazao wa wana wa Mungu na wabinti za wanadamu. Hao ndio watu waliokuwa mashujaa na wenye sifa wa zamani, na waliitwa Wanefili.
5Yawe alipoona uwingi wa uovu wa watu katika dunia, na kwamba kila kitu mwanadamu anachokusudia ndani ya moyo wake ni kiovu siku zote, 6Yawe akasikitika sana kwa kumwumba mwanadamu katika dunia. Yawe akahuzunika sana ndani ya moyo wake. 7Hivyo akasema: “Nitamuharibu kabisa katika dunia mwanadamu niliyemwumba, pamoja na nyama wa pori, viumbe vinavyotambaa na ndege wa anga. Ninasikitika kwamba niliwaumba katika dunia.” 8Lakini Noa akapata kukubaliwa mbele ya Yawe.
Noa
9Hizi ndizo habari za Noa na uzao wake. Noa alikuwa mwenye haki na mukamilifu kati ya watu wa wakati ule. Aliishi katika ushirika na Mungu. 10Noa alikuwa na wana watatu: Semu, Hamu na Yafeti. 11Mungu aliona kwamba dunia imeharibika na kujaa mateso makali. 12Mungu aliangalia dunia, akaona kwamba imeharibika kabisa, kwa maana kila mutu alifuata njia yake mbaya.
13Mungu akamwambia Noa: “Nimeamua kuwaangamiza wanadamu wote kwa sababu wamejaza dunia mateso makali. Hakika, nitawaangamiza kabisa pamoja na dunia! 14Kwa hiyo, ujitengenezee chombo kwa mbao ngumu. Gawanya vyumba ndani yake na ukipakae kabulimbo ndani na inje. 15Utakitengeneza hivi: urefu wake metre mia moja makumi tatu na tatu, upana wake metre makumi mbili na mbili na urefu wake kwenda juu metre kumi na tatu. 16Chombo hicho kikuwe cha gorofi tatu na chenye mulango pembeni. Utengeneze paa,#6.16 paa: au: dirisha. kisha uache nafasi ya karibu nusu metre kati ya paa na dari. 17Nitaleta mafuriko ya maji kwa kuangamiza viumbe vyote vyenye uzima katika dunia. Kila kiumbe chenye uzima katika dunia kitakufa. 18Lakini nitafanya agano nawe. Utaingia katika chombo, wewe pamoja na muke wako, wana wako na wake zao. 19Nawe utaingiza katika chombo kila aina ya viumbe, wawiliwawili, dume na dike, kwa kuwalinda wazima pamoja nawe.
20“Utaingiza kila aina ya ndege wa anga, kila aina ya nyama, kila aina ya kiumbe kinachotambaa, wawili wa kila aina, kwa kuwalinda wazima. 21Utwae vilevile aina zote za vyakula vinavyokuliwa, uvilinde kwa ajili ya chakula chenu na viumbe hivyo.” 22Noa akafanya yote kama vile Mungu alivyomwamuru.

Currently Selected:

Mwanzo 6: SWC02

Highlight

Share

Copy

None

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in