Mwanzo 34
34
Simeoni na Lawi wanalipiza kisasi kwa ajili ya dada yao
1Siku moja Dina, binti ya Yakobo na Lea, akakwenda kuwatembelea wanawake wa inchi hiyo. 2Basi, Sekemu mwana wa Hamori Muhivi, aliyekuwa mukubwa wa inchi hiyo, alipomwona Dina, akamushika, akalala naye kwa nguvu. 3Lakini Sekemu akavutiwa sana na yule binti, akamupenda hata akaanza kumubembeleza. 4Kwa hiyo, Sekemu akazungumuza na Hamori baba yake, akamwambia: “Unitwalie binti huyo kuwa muke wangu.”
5Yakobo akapata habari kwamba Sekemu amemuchafua binti yake Dina; lakini kwa sababu wana wake walikuwa pamoja na nyama kwenye malisho, akanyamaza mpaka waliporudi. 6Hamori, baba ya Sekemu, akakwenda kwa Yakobo kusudi azungumuze naye, 7na wakati uleule wana wa Yakobo walirudi kwa nyumba kutoka kwenye malisho. Waliposikia hayo, vijana wale wakaona uchungu mwingi na kukasirika sana, kwa vile Sekemu alikuwa amewafanyia watu wa Israeli ovu hilo la kulala na binti ya Yakobo; maana jambo hilo halipaswi kutendwa.
8Lakini Hamori akawaambia: “Mwana wangu Sekemu anamupenda sana binti yenu. Basi, tafazali mumuruhusu amwoe. 9Muache tuoeane: ninyi mutuoeshee wabinti zenu, nanyi muoe wabinti zetu. 10Kwa hiyo mutaishi pamoja nasi; mutakuwa huru katika inchi hii. Mutaishi humu, mufanye biashara na kujipatia mali.”
11Vilevile, Sekemu akawaambia baba na wandugu za Dina: “Ninataka kukubaliwa mbele yenu, nami nitawapa ninyi chochote mutakachosema. 12Muniombe mali na zawadi, hata ikiwa kikubwa namna gani, nami nitatoa, kufuatana na jinsi mutakavyoniambia. Lakini munipatie tu binti huyu kuwa muke wangu.”
13Basi, wana wa Yakobo wakamujibu Sekemu na baba yake Hamori kwa udanganyifu, kwa sababu Sekemu alikuwa amekwisha kumuchafua dada yao Dina. 14Wakawaambia: “Hatuwezi kumwoesha dada yetu kwa mutu asiyetahiriwa. Kufanya hivyo ni haya kwetu. 15Tutakubaliana nanyi tu kwa sharti hili: kwamba mutakuwa kama sisi kwa kumutahiri kila mwanaume kati yenu. 16Kwa hiyo tutawaoeshea wabinti zetu na kuwaoa wabinti zenu. Tutaishi pamoja nanyi na kuwa jamaa moja. 17Lakini musipokubaliana nasi na kutahiriwa, basi, sisi tutamutwaa binti yetu na kujiendea yetu.”
18Pendekezo lao likapendeza Hamori na mwana wake Sekemu. 19Kijana yule hakusita hata kidogo kutimiza sharti hilo, kwa vile alivyomupenda binti ya Yakobo, ingawa ni yeye ndiye aliyeheshimika kuliko wote katika nyumba yao.
20Basi, Hamori na mwana wake Sekemu, wakakwenda kwenye mulango wa muji, pahali pa mikutano, wakaongea na watu wao wakisema: 21“Watu hawa ni warafiki zetu. Tuwakaribishe waishi katika inchi yetu na kufanya biashara, kwa sababu tuko na inchi ya kututosha sisi na wao vilevile; kisha tutaoa wabinti zao na kuwaoshea binti wetu. 22Lakini wao watakubali kuishi nasi na tutakuwa jamaa moja kwa sharti hili: kwamba tutamutahiri kila mwanaume kati yetu kama vile wao walivyotahiriwa. 23Hamuoni kwamba nyama wao wa kufugwa na mali yao yote itakuwa mali yetu? Basi, tukubaliane nao kusudi wakae pamoja nasi.” 24Wanaume wote waliokusanyika kwenye mulango wa muji ule wakakubaliana na Hamori na mwana wake Sekemu. Kisha, wanaume wote wakatahiriwa.
25Kisha siku tatu, waliotahiriwa wakiwa wangali na maumivu makali, wana wawili wa Yakobo, Simeoni na Lawi, kaka za Dina, wakatwaa panga zao, wakashambulia muji kwa rafla na kuwaua wanaume wote. 26Wakawaua kwa upanga Hamori na mwana wake Sekemu, wakamutoa Dina katika nyumba ya Sekemu, wakajiendea. 27Nyuma ya mauaji hayo, wana wengine wa Yakobo wakaingia katika muji na kunyanganya mali yote katika muji ule, kwa sababu dada yao alikuwa amechafuliwa. 28Walitwaa kondoo na mbuzi, ngombe, punda na chochote kilichokuwa katika muji au katika shamba. 29Walitwaa mali yote, watoto na wanawake wote na chochote kilichokuwa ndani ya nyumba zao.
30Basi, Yakobo akamwambia Simeoni na Lawi: “Ninyi mumeniletea taabu kwa kunifanya nichukiwe na wakaaji wa inchi hii ya Wakanana na Waperizi. Mimi sina watu wengi, na kama wakikusanyika kwa kunishambulia wataniangamiza mimi pamoja na jamaa yangu.”
31Hao wandugu wawili wakajibu: “Ana haki gani ya kumutendea dada yetu kama kahaba?”
Currently Selected:
Mwanzo 34: SWC02
Highlight
Share
Copy

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.