YouVersion Logo
Search Icon

Yohane 8

8
1lakini Yesu akaenda kwenye mlima wa Mizeituni.#8:1 Mlima wa mizeituni: Upande wa mashariki ya mji wa Yerusalemu, kupita Bonde la Kidroni. Unaitwa Mlima wa Mizeituni kutokana na mizeituni mingi iliyoota kwenye miteremko yake. 2Kesho yake asubuhi na mapema alikwenda tena hekaluni. Watu wote wakamwendea, naye akaketi akawa anawafundisha. 3Basi, waalimu wa sheria na Mafarisayo wakamletea mwanamke mmoja aliyefumaniwa katika uzinzi. Wakamsimamisha katikati yao. 4Kisha wakamwuliza Yesu, “Mwalimu! Mwanamke huyu alifumaniwa katika uzinzi. 5Katika sheria yetu Mose alituamuru mwanamke kama huyu apigwe mawe.#8:5 Mwanamke kama huyu apigwe mawe: Katika sheria ya Mose (Lawi 20:10,22 na Kumb 22:22-24) mwanamke aliyefumaniwa akilala na mwanamume asiye mume wake, yeye na huyo mwanamume, walitakiwa wauawe kwa kupigwa mawe. Lakini hapa ni huyu mama tu anatajwa. Wale mashahidi walitakiwa wawe wa kwanza kabisa kumpiga mawe (aya 7). Basi, wewe wasemaje?” 6Walisema hivyo kumjaribu,#8:6 Kumjaribu: Taz pia mazingira ya maswali ya kutega au yenye utata katika Mat 22:15-22 na sambamba. Kuna njia mbili tu za kukabili suala hilo: au Yesu ataitupilia mbali sheria ya Mose, au atakubali huyo mama auawe. wapate kisa cha kumshtaki. Lakini Yesu akainama chini, akaandika ardhini kwa kidole. 7Walipozidi kumwuliza, Yesu akainuka, akawaambia, “Mtu asiye na dhambi miongoni mwenu na awe wa kwanza kumpiga jiwe.” 8Kisha akainama tena, akawa anaandika ardhini. 9Waliposikia hivyo, wakaanza kutoweka mmojammoja, wakitangulia wazee. Yesu akabaki peke yake, na yule mwanamke amesimama palepale. 10Yesu alipoinuka akamwuliza huyo mwanamke, “Wako wapi wale watu? Je, hakuna hata mmoja aliyekuhukumu?” 11Huyo mwanamke akamjibu, “Bwana, hakuna hata mmoja!” Naye Yesu akamwambia, “Wala mimi sikuhukumu. Nenda zako; na tangu sasa usitende dhambi tena.”]
Yesu mwanga wa ulimwengu
12Yesu alipozungumza nao tena, aliwaambia, “Mimi ndimi mwanga wa ulimwengu.#8:12 Mimi ndimi mwanga wa ulimwengu: Yesu anatetea ukweli wa ujumbe wake na kwamba amekuja ulimwenguni kusudi watu waone jinsi Mungu alivyo. Itakumbukwa pia kwamba katika Mat 5:14 wale wanafunzi wake pia wanasemwa kuwa ni mwanga wa ulimwengu. Taz pia Yoh 9:5. Anayenifuata mimi hatembei kamwe gizani, bali atakuwa na mwanga wa uhai.”
13Basi, Mafarisayo wakamwambia, “Wewe unajishuhudia mwenyewe; kwa hiyo ushahidi wako si halali.” 14Yesu akawajibu, “Hata kama ninajishuhudia mwenyewe, ushahidi wangu ni wa kweli kwa sababu mimi najua nilikotoka na ninakokwenda. Lakini nyinyi hamjui nilikotoka wala ninakokwenda. 15Nyinyi mnahukumu kwa fikira za kibinadamu, lakini mimi simhukumu mtu. 16Hata nikihukumu, hukumu yangu ni halali kwa sababu mimi siko peke yangu; Baba aliyenituma yuko pamoja nami. 17Imeandikwa katika sheria yenu ya kwamba ushahidi wa watu wawili ni halali. 18Mimi najishuhudia mwenyewe, naye Baba aliyenituma, ananishuhudia pia.” 19Hapo wakamwuliza, “Baba yako yuko wapi?” Yesu akawajibu, “Nyinyi hamnijui mimi wala hammjui Baba. Kama mngenijua mimi, mngemjua na Baba yangu pia.”
20Yesu alisema maneno hayo kwenye chumba cha hazina#8:20 Chumba cha hazina: Huenda mahali hapo palikuwa katika ukumbi wa wanawake, karibu na mahali palipokuwa na vijisanduku vya kuweka sadaka. Taz Luka 21:1. alipokuwa anafundisha hekaluni. Wala hakuna mtu aliyemtia nguvuni, kwa sababu saa yake ilikuwa haijafika bado.#8:20 Saa yake ilikuwa haijafika bado: Taz 2:4 maelezo.
Niendako nyinyi hamwezi kufika
21Yesu akawaambia tena, “Naenda zangu nanyi mtanitafuta, lakini mtakufa katika dhambi zenu.#8:21 Mtakufa katika dhambi zenu: Yaani watakufa wakiwa hawajaachana na dhambi zao au hawajasamehewa (taz pia aya ya 24; ling Kumb 6:23; 8:10). Niendako mimi, nyinyi hamwezi kufika.” 22Basi, viongozi wa Wayahudi wakasema, “Je, atajiua? Mbona anasema: ‘Niendako nyinyi hamwezi kufika?’” 23Yesu akawaambia, “Nyinyi mmetoka papa hapa chini, mimi nimetoka juu; nyinyi ni wa ulimwengu huu, mimi si wa ulimwengu#8:23 Nyinyi mmetoka …hapa chini, mimi nimetoka juu; nyinyi ni wa ulimwengu mimi si wa ulimwengu: Yesu anadokezea kwa maneno hayo kwamba yeye ametoka kwa Mungu. Lakini pia matumizi ya “ulimwengu” ambako hao wanaompinga wametoka ni ya kimfano kuelezea eneo ambalo katika Maandiko Matakatifu ni eneo la wenye kumpinga Mungu (15:18-19; Gal 6:14). huu. 24Ndiyo maana niliwaambieni mtakufa katika dhambi zenu. Kama msipoamini kwamba ‘Mimi Ndimi#8:24 Mimi ndimi: Maneno ambayo, kulingana na maana yake, karibu ni sawa na yale yaliyotumiwa katika Kut 3:14 pale Mungu alipojitambulisha kwa Mose na watu wa Israeli kama “Mimi Ndimi”. Katika sehemu hiyo ya Kut 3 Mwenyezi-Mungu (Kiebrania: “Yahweh”) ndiye aliye kweli au ndiye mwenye kusababisha kuweko. Yaani yewye ni chanzo cha chochote kilichopo. Katika Injili ya Yohane Yesu anatumia msemo huo kujiunga na dhana au mawazo hayo juu ya Mungu na kueleza yale ambayo Mungu alimwagiza ayatekeleze ulimwenguni. Niliye’, mtakufa katika dhambi zenu.” 25Nao wakamwuliza, “Wewe ni nani?” Yesu akawajibu, “Nimewaambieni tangu mwanzo!#8:25 Nimewaambieni tangu mwanzo: Au: “Ya nini hata niongee nanyi?” 26Ninayo mengi ya kusema na kuhukumu juu yenu. Lakini yule aliyenituma ni kweli; nami nauambia ulimwengu mambo yale tu niliyoyasikia kutoka kwake.”
27Hawakuelewa kwamba Yesu alikuwa akisema nao juu ya Baba. 28Basi, Yesu akawaambia, “Mtakapokwisha mwinua Mwana wa Mtu,#8:28 Mtakapokwisha mwinua Mwana wa Mtu: Wazo linalogusiwa hapa ni lile la kifo cha Yesu msalabani (taz Yoh 3:14). Katika 3:14 Yesu anasema atainuliwa juu kama Mose alipoinua juu yule nyoka wa shaba kusudi waliotazama nyoka huyo waweze kuponywa, na kwa namna hiyo hiyo wale wanaomtazama Yesu katika hali yake ya kuinuliwa juu msalabani wataweza nao kuponywa. hapo ndipo mtakapojua kwamba ‘Mimi Ndimi Niliye’,#8:28 Mimi Ndimi Niliye: Taz 8:24 maelezo. na kwamba sifanyi chochote mimi mwenyewe, ila nasema tu yale Baba aliyonifundisha. 29Yule aliyenituma yuko pamoja nami; yeye hakuniacha peke yangu kwani nafanya daima yale yanayompendeza.” 30Baada ya kusema hayo watu wengi walimwamini.
Ukweli utawapeni uhuru#8:31-47 Ukweli utawapeni uhuru: Huo ukweli sio ukweli wa jumla ila ni ukweli juu ya Mungu na ambao ulifunuliwa na Yesu Kristo (14:6). Ukweli huu unajulikana kwa wale wanaomtii Yesu na mafundisho yake. Uhuru unaotajwa hapa si uhuru wa kutotawaliwa na watu wengine ila ni uhuru ule wa kiroho wa kutotawaliwa na dhambi, kama inavyosemwa katika aya 34.
31Basi, Yesu akawaambia wale Wayahudi waliomwamini, “Kama mkiyazingatia mafundisho yangu mtakuwa kweli wanafunzi wangu. 32Mtaujua ukweli, nao ukweli utawapeni uhuru.” 33Nao wakamjibu, “Sisi ni wazawa wa Abrahamu, na hatujapata kamwe kuwa watumwa wa mtu yeyote yule. Una maana gani unaposema: ‘Mtakuwa huru?’” 34Yesu akawajibu, “Kweli nawaambieni, kila mtu anayetenda dhambi ni mtumwa wa dhambi.#8:34 Kila mtu anayetenda dhambi ni mtumwa wa dhambi: Baadhi ya hati za kale zina: Kila mtu atendaye dhambi ni mtumwa. 35Mtumwa hana makao ya kudumu nyumbani, lakini mwana anayo makao ya kudumu. 36Mwana akiwapeni uhuru mtakuwa huru kweli. 37Najua kwamba nyinyi ni wazawa wa Abrahamu. Hata hivyo, mnataka kuniua kwa sababu hamyakubali mafundisho yangu. 38Mimi nasema yale aliyonionesha Baba, lakini nyinyi mwafanya yale aliyowaambieni baba yenu.”
39Wao wakamjibu, “Sisi ni watoto wa Abrahamu!” Yesu akawaambia, “Kama nyinyi mngekuwa watoto wa Abrahamu, mngefanya kama alivyofanya Abrahamu. 40Mimi nimewaambieni ukweli niliousikia kwa Mungu; hata hivyo, nyinyi mwataka kuniua. Abrahamu hakufanya hivyo! 41Nyinyi mnafanya mambo yaleyale aliyofanya baba yenu.” Wao wakamwambia, “Sisi si watoto haramu! Tunaye baba mmoja tu, yaani Mungu.” 42Yesu akawaambia, “Kama Mungu angekuwa Baba yenu, mngenipenda mimi, maana mimi nilitoka kwa Mungu na sasa niko hapa. Sikuja kwa mamlaka yangu mwenyewe, ila yeye alinituma. 43Kwa nini hamuelewi hayo ninayosema? Ni kwa kuwa hamuezi kuusikiliza ujumbe wangu. 44Nyinyi ni watoto wa baba yenu Ibilisi#8:44 Nyinyi ni watoto wa baba yenu Ibilisi: Maneno haya ni upeo wa ubishi kati ya Yesu na hao waliotajwa katika aya ya 30. Ibilisi au Shetani ni kiongozi wa nguvu zote zinazopingana na Mungu. Yesu alikuja ulimwenguni kushinda nguvu hizo za Shetani au Ibilisi. na mnataka tu kutekeleza tamaa za baba yenu. Yeye alikuwa muuaji tangu mwanzo; hana msimamo katika ukweli, kwani ukweli haumo ndani yake. Kila asemapo uongo, husema kutokana na hali yake ya maumbile, maana yeye ni mwongo na baba wa uongo. 45Mimi nasema ukweli, na ndiyo maana nyinyi hamniamini. 46Nani kati yenu awezaye kuthibitisha kuwa mimi nina dhambi? Ikiwa basi nasema ukweli, kwa nini hamniamini? 47Aliye wa Mungu husikiliza maneno ya Mungu. Lakini nyinyi hamsikilizi kwa sababu nyinyi si watu wa Mungu.”
Yesu alikuwako kabla ya Abrahamu
48Wayahudi wakamwambia, “Je, hatukusema kweli kwamba wewe ni Msamaria,#8:48 Wewe ni Msamaria: Walitumia msemo huo kwa kumdharau kwani Wayahudi na Wasamaria hawakushirikiana. na tena una pepo?” 49Yesu akajibu, “Mimi sina pepo; mimi namheshimu Baba yangu, lakini nyinyi hamniheshimu. 50Mimi sijitafutii utukufu wangu mwenyewe; yuko mmoja mwenye kuutafuta utukufu huo, naye ni hakimu. 51Kweli nawaambieni, anayeuzingatia ujumbe wangu hatakufa milele.” 52Basi, Wayahudi wakasema, “Sasa tunajua kweli kwamba wewe una pepo! Abrahamu alikufa, na manabii pia walikufa,#8:52 Abrahamu alikufa, na manabii pia walikufa: Hapa ni dhahiri watu hawakuelewa maana ya yale aliyosema Yesu kwamba hawatakufa kama wakimtii yeye. Walifikiri kwamba alikuwa anasema juu ya kuishi daima hapa duniani. Tazama 3:4 ambapo pana kutokuelewa kwa namna hiyo hiyo. nawe wasema ati, ‘Anayeuzingatia ujumbe wangu hatakufa milele!’ 53Je, unajifanya mkuu kuliko baba yetu Abrahamu ambaye alikufa? Hata na manabii walikufa. Wewe unajifanya kuwa nani?” 54Yesu akawajibu, “Nikijitukuza mwenyewe, utukufu wangu si kitu. Baba yangu ambaye nyinyi mwasema ni Baba yenu, ndiye anayenitukuza. 55Nyinyi hamjapata kumjua, lakini mimi namjua. Na, nikisema simjui, nitakuwa mwongo kama nyinyi. Mimi namjua na ninashika neno lake. 56Abrahamu, baba yenu, alishangilia aione siku yangu; naye aliiona, akafurahi.” 57Basi, Wayahudi wakamwambia, “Wewe hujatimiza miaka hamsini bado, nawe umemwona Abrahamu?”#8:57 Umemwona Abrahamu?: Baadhi ya hati za kale zina: Abrahamu amekuona? 58Yesu akawaambia, “Kweli nawaambieni, kabla Abrahamu hajazaliwa, mimi niko.”#8:58 Kabla ya Abrahamu hajazaliwa, mimi niko: Au: “Mimi ndimi” kama 8:24. 59Hapo wakaokota mawe ili wamtupie, lakini Yesu akajificha, akatoka hekaluni.

Currently Selected:

Yohane 8: BHNTLK

Highlight

Share

Copy

None

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in

YouVersion uses cookies to personalize your experience. By using our website, you accept our use of cookies as described in our Privacy Policy