YouVersion Logo
Search Icon

1 Wafalme 18

18
Ujumbe wa Eliya kwa Ahabu
1 # Lk 4:25; Yak 5:17; Kum 28:12 Ikawa baada ya siku nyingi, neno la BWANA likamjia Eliya, katika mwaka wa tatu, kusema, Nenda, ukajioneshe kwa Ahabu; nami nitaleta mvua juu ya nchi. 2Basi Eliya akaenda ili ajioneshe kwa Ahabu. Na njaa ilikuwa nzito katika Samaria. 3#Neh 7:2; Ayu 28:28 Ahabu akamwita Obadia, aliyekuwa juu ya nyumba yake; (na huyu Obadia alikuwa mwenye kumcha BWANA sana; 4#Mt 10:40-42 kwa kuwa ikawa, Yezebeli alipowaua manabii wa BWANA, Obadia akatwaa manabii mia moja, akawaficha hamsini hamsini katika pango, akawalisha chakula na kuwapa maji). 5Ahabu akamwambia Obadia, Pita katika nchi, kwenye chemchemi zote za maji, na vijito vyote; labda tutapata majani, tuwahifadhi hai farasi na nyumbu, tusipate hasara ya hao wanyama wote. 6Basi wakaigawanya nchi, ili wapite katika nchi yote; Ahabu akaenda zake njia moja peke yake, na Obadia akaenda zake njia nyingine peke yake. 7Na Obadia alipokuwa njiani, kumbe! Eliya akakutana naye. Akamtambua, akaanguka kifudifudi, akanena, Je! Ni wewe, bwana wangu Eliya? 8Akamjibu, Ni mimi. Nenda, umwambie bwana wako, Tazama, Eliya yupo. 9Akamwambia, Nimekosa nini, hata unitie mimi mtumishi wako mkononi mwa Ahabu, aniue? 10Kama BWANA, Mungu wako, aishivyo, hakuna taifa wala ufalme ambao bwana wangu hakutuma watu wakutafute; na waliposema, Hayupo, akawaapisha ule ufalme, na taifa, ya kwamba hawakukuona. 11Nawe sasa wasema, Nenda, umwambie bwana wako, Tazama, Eliya yupo. 12#2 Fal 2:16; Eze 3:12,14; Mt 4:1; Mdo 8:39 Na itakuwa, mara mimi nikiondoka kwako, Roho ya BWANA atakuchukua uende nisikojua; nami nitakapokwenda kumwambia Ahabu, naye asipokuona, ataniua, lakini mimi mtumishi wako namcha BWANA tangu ujana wangu. 13Je! Bwana wangu hakuambiwa nilivyofanya hapo Yezebeli alipowaua manabii wa BWANA? Jinsi nilivyowaficha manabii wa BWANA, watu mia moja, hamsini hamsini katika pango, nikawalisha chakula na kuwapa maji? 14Nawe sasa wasema, Nenda umwambie bwana wako, Tazama, Eliya yupo; basi, ataniua. 15Eliya akasema, Kama BWANA wa majeshi aishivyo ambaye ninasimama mbele zake, hakika nitajionesha kwake leo. 16Basi, Obadia akaenda zake amwone Ahabu, akamwambia; naye Ahabu akaenda kumlaki Eliya.
17 # 1 Fal 21:20; Yos 7:25; Lk 23:2; Mdo 16:20 Ikawa, Ahabu alipomwona Eliya, Ahabu akamwambia, Je! Ni wewe, Ewe mtaabishaji wa Israeli? 18#1 Fal 9:9; 2 Nya 15:2; 24:20 Naye akajibu, Si mimi niliyewataabisha Israeli; bali ni wewe, na nyumba ya baba yako, kwa kuwa mmeziacha amri za BWANA; nawe umewafuata mabaali. 19#Yos 19:26; Yer 46:18; 1 Fal 16:33 Basi sasa upeleke watu, unikusanyie jamii ya Israeli katika mlima wa Karmeli, na wale manabii wa Baali mia nne na hamsini, na wale manabii wa Ashera mia nne, walao chakula mezani pa Yezebeli.
Eliya awashinda makuhani wa Baali
20 # 1 Fal 22:6 Basi, Ahabu akapeleka watu kwa wana wa Israeli wote, akawakusanya manabii pamoja katika mlima wa Karmeli.
21 # 2 Fal 17:41; Mt 6:24; 1 Kor 10:21,22; Ufu 3:15; Yos 24:15; Zab 100:3 Naye Eliya akawakaribia watu wote, akanena, Mtasitasita katikati ya mawazo mawili hata lini? BWANA akiwa ndiye Mungu, mfuateni; bali ikiwa Baali ni Mungu, haya! Mfuateni yeye. Wale watu hawakumjibu neno. 22#1 Fal 19:10,14 Ndipo Eliya akawaambia watu, Mimi nimesalia, mimi peke yangu, nabii wa BWANA; lakini manabii wa Baali ni watu mia nne na hamsini. 23Kwa hiyo na watutolee ng'ombe wawili; wao na wajichagulie ng'ombe mmoja, wamkatakate na kumweka juu ya kuni, wasitie moto chini; nami nitamtengeza huyo ng'ombe wa pili, na kumweka juu ya kuni, wala sitatia moto chini. 24#Law 9:24; 1 Nya 21:26; 2 Nya 7:1 Nanyi ombeni kwa jina la mungu wenu, nami nitaomba kwa jina la BWANA; na Mungu yule ajibuye kwa moto, na awe ndiye Mungu. Watu wote wakajibu wakasema, Maneno haya ni mazuri. 25Eliya akawaambia manabii wa Baali, Jichagulieni ng'ombe mmoja, mkamtengeze kwanza; maana ninyi ndio wengi; mkaliitie jina la mungu wenu, wala msitie moto chini. 26#Zab 115:5; Yer 10:5; 1 Kor 8:4; 12:2 Wakamtwaa yule ng'ombe waliyepewa, wakamtengeza, wakaliitia jina la Baali tangu asubuhi hata adhuhuri, wakisema, Ee Baali, utusikie. Lakini hapakuwa na sauti, wala aliyejibu. Nao wakarukaruka juu ya madhabahu waliyoifanya. 27Ikawa, wakati wa adhuhuri, Eliya akawafanyia dhihaka, akasema, Mwiteni kwa sauti kuu; maana ni mungu huyo; labda anazungumza, au ana shughuli, au anasafiri, au labda amelala, sharti aamshwe. 28#Law 19:28; Kum 14:1 Wakapiga kelele, wakajikatakata kwa visu na vyembe kama ilivyo desturi yao, hata damu ikawachuruzika. 29#1 Kor 11:4,5 Ikawa, wakati wa adhuhuri ulipopita, walitabiri hata wakati wa kutoa dhabihu ya jioni; lakini hapakuwa na sauti, wala aliyejibu, wala aliyeangalia.
30Kisha Eliya akawaambia watu wote, Nikaribieni mimi. Watu wote wakamkaribia. Akaitengeneza madhabahu ya BWANA iliyovunjika. 31#Mwa 32:28; 35:10; 2 Fal 17:34 Eliya akatwaa mawe kumi na mawili, kwa hesabu ya makabila ya wana wa Yakobo, aliyejiliwa na neno la BWANA na kuambiwa, Jina lako litakuwa Israeli. 32#Kol 3:17 Naye akaijenga madhabahu kwa mawe hayo katika jina la BWANA; akafanya mfereji, kama wa vipimo viwili vya mbegu, ukiizunguka madhabahu. 33#Law 1:6; Amu 6:20 Kisha akazipanga zile kuni, akamkata yule ng'ombe vipande vipande, akaviweka juu ya kuni. Akasema, Jazeni mapipa manne maji, mkayamwage juu ya sadaka ya kuteketezwa, na juu ya kuni. 34Akasema, Fanyeni mara ya pili. Wakafanya mara ya pili. Akasema, Fanyeni mara ya tatu. Wakafanya mara ya tatu. 35Yale maji yakaizunguka madhabahu; akaujaza mfereji maji.
36 # Kut 29:39; Mwa 28:13; Kut 3:6; 4:5; Mt 22:32; Ebr 11:16; 1 Fal 8:43; 2 Fal 19:19; Zab 83:18; Hes 16:28 Ikawa, wakati wa kutoa dhabihu ya jioni, Eliya nabii akakaribia, akasema, Ee BWANA, Mungu wa Abrahamu, na wa Isaka, na wa Israeli, na ijulikane leo ya kuwa wewe ndiwe Mungu katika Israeli, na ya kuwa mimi ni mtumishi wako, na ya kuwa nimefanya mambo haya yote kwa neno lako. 37#Yer 10:23; 31:18 Unisikie, Ee BWANA, unisikie, ili watu hawa wajue ya kuwa wewe, BWANA, ndiwe Mungu, na ya kuwa wewe umewageuza moyo wakurudie. 38#Law 9:24; Amu 6:21; 1 Nya 21:26; 2 Nya 7:1 Ndipo moto wa BWANA ukashuka, ukaiteketeza sadaka ya kuteketezwa, na kuni, na mawe, na mavumbi, ukayaramba yale maji yaliyokuwamo katika mfereji. 39Na watu wote walipoona, wakaanguka kifudifudi; wakasema, BWANA ndiye Mungu, BWANA ndiye Mungu. 40#2 Fal 10:25; Kum 13:5; 18:20; Ufu 19:20 Eliya akawaambia, Wakamateni hao manabii wa Baali, asiokoke hata mmoja. Wakawakamata; na Eliya akawachukua mpaka kijito cha Kishoni, akawaua huko.
Mwisho wa ukame
41Naye Eliya akamwambia Ahabu, Haya! Inuka, ule, unywe; kwani pana sauti ya mvua tele. 42#Yak 5:17 Basi Ahabu akainuka ili ale na kunywa. Naye Eliya akapanda juu mpaka kilele cha Karmeli; akasujudu kifudifudi, akainama uso mpaka magotini. 43#Mwa 32:20; Hab 2:3 Akamwambia mtumishi wake, Kwea sasa, utazame upande wa bahari. Akakwea, akatazama, na kusema, Hakuna kitu. Naye akanena, Nenda tena mara saba. 44Ikawa mara ya saba akasema, Tazama, wingu linatoka katika bahari, nalo ni dogo kama mkono wa mtu. Akanena, Nenda, umwambie Ahabu, Tandika, ushuke, mvua isikuzuie. 45Ikawa, muda si muda, mbingu zikawa nyeusi kwa mawingu na upepo, ikanyesha mvua nyingi. Ahabu akapanda garini, akaenda zake Yezreeli. 46#2 Fal 3:15; Eze 1:3; 3:14 Mkono wa BWANA ulikuwa juu ya Eliya; akajikaza viuno, akapiga mbio akatangulia Ahabu mpaka kuiingia Yezreeli.

Currently Selected:

1 Wafalme 18: SRUV

Highlight

Share

Copy

None

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in