Zaburi 32:1-11
Zaburi 32:1-11 Biblia Habari Njema (BHN)
Heri yake mtu aliyesamehewa kosa lake, mtu ambaye dhambi yake imeondolewa kabisa. Heri mtu ambaye Mwenyezi-Mungu hamwekei hatia, mtu ambaye hana hila moyoni mwake. Wakati nilipokuwa sijakiri dhambi yangu, nilikuwa nimedhoofika kwa kulia mchana kutwa. Mchana na usiku mkono wako ulinilemea; nikafyonzwa nguvu zangu, kama maji wakati wa kiangazi. Kisha nilikiri makosa yangu kwako; wala sikuuficha uovu wangu. Nilisema ninakuungamia makosa yangu ee Mwenyezi-Mungu, ndipo nawe ukanisamehe dhambi zangu zote. Kwa hiyo, kila mwaminifu na akuletee maombi; jeshi likaribiapo au mafuriko, hayo hayatamfikia yeye. Wewe ndiwe kinga yangu; wewe wanilinda katika taabu. Umenijalia shangwe za kukombolewa. Mungu asema: “Nitakufunza na kukuonesha njia unayopaswa kufuata. Nitakushauri kwa uangalifu mkubwa. Usiwe mpumbavu kama farasi au nyumbu, ambao lazima wafungwe lijamu na hatamu, la sivyo hawatakukaribia.” Watu waovu watapata mateso mengi, bali wanaomtumainia Mwenyezi-Mungu wazungukwa na fadhili zake. Furahini na kushangilia kwa sababu ya Mwenyezi-Mungu enyi waadilifu; pigeni vigelegele vya shangwe enyi wanyofu wa moyo.
Zaburi 32:1-11 Swahili Revised Union Version (SRUV)
Heri aliyesamehewa dhambi, Na kuondolewa makosa yake. Heri ambaye BWANA hamhesabii hatia, Na ambaye rohoni mwake hamna hila. Nilipokosa kuungama dhambi zangu, mifupa yangu ilipooza Kwa kulia kwangu mchana kutwa. Kwa maana mchana na usiku Mkono wako ulinilemea. Jasho langu likakauka hata nikawa Kama nchi kavu wakati wa kaskazi. Ndipo nikakuungamia dhambi yangu, Wala sikuuficha upotovu wangu. Nilisema, Nitayakiri maasi yangu kwa BWANA, Nawe ukanisamehe upotovu wa dhambi yangu. Kwa hiyo, hebu kila akuaminiye Akuombe awapo katika dhiki. Hakika maji makuu yafurikapo, Hayatamfikia yeye. Kimbilio langu utanilinda nisipate mateso, Utanizungusha nyimbo za kufurahia wokovu wangu. Nitakufundisha na kukuonesha njia utakayoiendea; Nitakushauri, jicho langu likikutazama. Msiwe kama farasi wala nyumbu, Wasiokuwa na akili. Kwa matandiko ya lijamu na hatamu Sharti kuwazuia hao, au hawatakukaribia. Naye mtu mwovu ana mapigo mengi, Bali amtumainiaye BWANA fadhili zitamzunguka. Mfurahieni BWANA; Shangilieni, enyi wenye haki Pigeni vigelegele vya furaha; Ninyi nyote mlio wanyofu wa moyo.
Zaburi 32:1-11 Maandiko Matakatifu ya Mungu Yaitwayo Biblia (SUV)
Heri aliyesamehewa dhambi, Na kusitiriwa makosa yake. Heri BWANA asiyemhesabia upotovu, Ambaye rohoni mwake hamna hila. Niliponyamaza mifupa yangu ilichakaa Kwa kuugua kwangu mchana kutwa. Kwa maana mchana na usiku Mkono wako ulinilemea. Jasho langu likakauka hata nikawa Kama nchi kavu wakati wa kaskazi. Nalikujulisha dhambi yangu, Wala sikuuficha upotovu wangu. Nalisema, Nitayakiri maasi yangu kwa BWANA, Nawe ukanisamehe upotovu wa dhambi yangu. Kwa hiyo kila mtu mtauwa Akuombe wakati unapopatikana. Hakika maji makuu yafurikapo, Hayatamfikia yeye. Ndiwe sitara yangu, utanihifadhi na mateso, Utanizungusha nyimbo za wokovu. Nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea; Nitakushauri, jicho langu likikutazama. Msiwe kama farasi wala nyumbu, Walio hawana akili. Kwa matandiko ya lijamu na hatamu Sharti kuwazuia hao, au hawatakukaribia. Naye mtu mwovu ana mapigo mengi, Bali amtumainiye BWANA fadhili zitamzunguka. Mfurahieni BWANA; Shangilieni, enyi wenye haki Pigeni vigelegele vya furaha; Ninyi nyote mlio wanyofu wa moyo.
Zaburi 32:1-11 Neno: Bibilia Takatifu (NEN)
Heri mtu yule ambaye amesamehewa makosa yake, ambaye dhambi zake zimefunikwa. Heri mtu yule ambaye BWANA hamhesabii dhambi, na ambaye rohoni mwake hamna udanganyifu. Niliponyamaza, mifupa yangu ilichakaa kwa kulia kwa maumivu makali mchana kutwa. Usiku na mchana mkono wako ulinilemea, nguvu zangu zilinyonywa kama vile katika joto la kiangazi. Kisha nilikujulisha dhambi yangu wala sikuficha uovu wangu. Nilisema, “Nitaungama makosa yangu kwa BWANA.” Ndipo uliponisamehe hatia ya dhambi yangu. Kwa hiyo kila mtu mcha Mungu akuombe wakati unapopatikana, hakika maji makuu yatakapofurika hayatamfikia yeye. Wewe ndiwe mahali pangu pa kujificha, utaniepusha na taabu na kunizunguka kwa nyimbo za wokovu. Nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea; nitakushauri na kukuangalia. Usiwe kama farasi au nyumbu wasio na akili, ambao ni lazima waongozwe kwa lijamu na hatamu la sivyo hawatakukaribia. Mtu mwovu ana taabu nyingi, bali upendo usio na kikomo wa BWANA unamzunguka mtu anayemtumaini. Shangilieni katika BWANA na mfurahi, enyi wenye haki! Imbeni, nyote mlio wanyofu wa moyo!