Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Zaburi 18:21-50

Zaburi 18:21-50 Biblia Habari Njema (BHN)

Maana nimefuata njia za Mwenyezi-Mungu, wala sikujitenga na Mungu wangu kwa uovu. Nimeshika maagizo yake yote, sikuacha kufuata masharti yake. Mbele yake sikuwa na hatia; nimejikinga nisiwe na hatia. Mwenyezi-Mungu amenituza kadiri ya uadilifu wangu; yeye ajua kwamba mikono yangu haina hatia. Wewe ni mwaminifu kwa walio waaminifu; mwema kwa wale walio wema. Wewe ni mkamilifu kwa walio wakamilifu; lakini mkatili kwa watu walio waovu. Wewe wawaokoa walio wanyenyekevu, lakini wenye majivuno huwaporomosha. Wewe ee Mwenyezi-Mungu, waniangazia; walifukuza giza langu, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wangu. Kwa msaada wako nakishambulia kikosi; wewe wanipa nguvu ya kuruka ukuta. Huyu Mungu matendo yake hayana dosari! Ahadi ya Mwenyezi-Mungu ni ya kuaminika; yeye ni ngao kwa wote wanaomkimbilia usalama. Nani aliye Mungu isipokuwa Mwenyezi-Mungu? Nani aliye mwamba wa usalama ila Mungu wetu? Mungu ndiye anijaliaye nguvu kila upande; ndiye anayeifanya salama njia yangu. Ameiimarisha miguu yangu kama ya paa, na kuniweka salama juu ya vilele. Hunifunza kupigana vita, mikono yangu iweze kuvuta upinde wa shaba. Umenipa ngao yako ya kuniokoa; mkono wako wa kulia umenitegemeza; wema wako umenifanikisha. Umenirahisishia njia yangu; wala miguu yangu haikuteleza. Niliwafuatia adui zangu na kuwakamata; sikurudi nyuma mpaka nimewaangamiza. Niliwaangusha chini wasiweze kuinuka tena; walianguka chini ya miguu yangu. Wewe ulinijalia nguvu ya kupigana vita; uliwaporomosha maadui chini yangu. Uliwafanya maadui zangu wakimbie, na wale walionichukia niliwaangamiza. Walipiga yowe lakini hapakuwa na wa kuwaokoa; walimlilia Mwenyezi-Mungu lakini hakuwajibu. Niliwatwanga wakawa kama vumbi inayopeperushwa na upepo; niliwakanyaga kama tope la njiani. Wewe uliniokoa na mashambulizi ya watu, ukanifanya mtawala wa mataifa. Watu nisiowajua walinitumikia. Mara waliposikia habari zangu walinitii. Wageni walinijia wakinyenyekea. Wageni walikufa moyo; wakaja kutoka ngome zao wakitetemeka. Mwenyezi-Mungu yu hai! Asifiwe mwamba wa usalama wangu; atukuzwe Mungu wa wokovu wangu. Yeye ameniwezesha kulipiza kisasi; na kuyashinda mataifa chini yangu. Ameniokoa kutoka kwa maadui zangu, akanikuza juu ya wapinzani wangu, na kunisalimisha mbali na watu wakatili. Kwa hiyo nitakutukuza kati ya mataifa, ee Mwenyezi-Mungu nitaliimbia sifa jina lako. Mungu humjalia mfalme wake ushindi mkubwa; humwonesha fadhili zake huyo mteule wake, naam, humfadhili Daudi na wazawa wake milele.

Shirikisha
Soma Zaburi 18

Zaburi 18:21-50 Swahili Revised Union Version (SRUV)

Maana nimezishika njia za BWANA, Wala sikumwasi Mungu wangu. Hukumu zake zote zilikuwa mbele yangu, Wala amri zake sikubandukana nazo. Nami nilikuwa mkamilifu mbele zake, Nikajilinda na uovu wangu. Ndipo BWANA akanilipa sawasawa na haki yangu, Sawasawa na usafi wa mikono yangu mbele zake. Kwa mtu mwenye fadhili utakuwa mwenye fadhili; Kwa mkamilifu utajionesha kuwa mkamilifu; Kwake ajitakasaye utajionesha kuwa mtakatifu; Na kwa mpotovu utajionesha kuwa mkaidi. Maana Wewe wawaokoa watu wanaoonewa, Na macho ya kiburi utayadhili. Kwa kuwa Wewe unaiwasha taa yangu; BWANA Mungu wangu aniangazia giza langu. Maana kwa msaada wako nafuatia jeshi, Kwa msaada wa Mungu wangu naruka ukuta. Mungu, njia yake ni kamilifu, Ahadi ya BWANA imehakikishwa, Yeye ndiye ngao yao. Wote wanaomkimbilia. Maana ni nani aliye Mungu ila BWANA? Ni nani aliye mwamba ila Mungu wetu? Mungu ndiye anifungaye mshipi wa nguvu, Naye anaifanya kamilifu njia yangu. Miguu yangu anaifanya kuwa ya kulungu, Na kunisimamisha mahali pangu pa juu. Anaifundisha mikono yangu vita, Mikono yangu ikaupinda upinde wa shaba. Nawe umenipa ngao ya wokovu wako, Mkono wako wa kulia umenitegemeza, Na unyenyekevu wako umenikuza. Umezipanulia nafasi hatua zangu, Na miguu yangu haikuteleza. Nitawafuatia adui zangu na kuwapata, Wala sitarudi nyuma hadi wakomeshwe. Nitawapigapiga wasiweze kusimama, Wataanguka chini ya miguu yangu. Nawe umenipa nguvu za vita, Hunitiishia chini yangu walionishambulia. Naam, adui zangu umewafanya wanipe visogo, Nao walionichukia nimewakatilia mbali. Walipiga yowe, lakini hakuna wa kuokoa, Walimwita BWANA lakini hakuwajibu, Nikawaponda kama mavumbi mbele ya upepo, Nikawatupa nje kama matope ya njiani. Umeniokoa kutoka kwa mashindano ya watu, Umenifanya niwe kichwa cha mataifa. Watu nisiowajua walinitumikia. Mara tu waliposikia habari zangu, wakanitii. Wageni walinijia wakinyenyekea. Wageni nao walitepetea, Walitoka katika ngome zao wakitetemeka. BWANA ndiye aliye hai; Na ahimidiwe mwamba wangu; Na atukuzwe Mungu wa wokovu wangu; Ndiye Mungu anilipizaye kisasi; Na kuwatiisha watu chini yangu. Huniponya na adui zangu; Naam, waniinua juu yao walioniinukia, Na kuniponya na mtu mjeuri. Basi, BWANA, nitakushukuru kati ya mataifa, Nami nitaliimbia jina lako. Ampa mfalme wake wokovu mkuu, Amfanyia fadhili masihi wake, Daudi na wazawa wake hata milele.

Shirikisha
Soma Zaburi 18

Zaburi 18:21-50 Maandiko Matakatifu ya Mungu Yaitwayo Biblia (SUV)

Maana nimezishika njia za BWANA, Wala sikumwasi Mungu wangu. Hukumu zake zote zilikuwa mbele yangu, Wala amri zake sikujiepusha nazo. Nami nalikuwa mkamilifu mbele zake, Nikajilinda na uovu wangu. Mradi BWANA amenilipa sawasawa na haki yangu, Sawasawa na usafi wa mikono yangu mbele zake. Kwa mtu mwenye fadhili utakuwa mwenye fadhili; Kwa mkamilifu utajionyesha kuwa mkamilifu; Kwake ajitakasaye utajionyesha kuwa mtakatifu; Na kwa mpotovu utajionyesha kuwa mkaidi. Maana Wewe utawaokoa watu wanaoonewa, Na macho ya kiburi utayadhili. Kwa kuwa Wewe unaiwasha taa yangu; BWANA Mungu wangu aniangazia giza langu. Maana kwa msaada wako nafuatia jeshi, Kwa msaada wa Mungu wangu naruka ukuta. Mungu, njia yake ni kamilifu, Ahadi ya BWANA imehakikishwa, Yeye ndiye ngao yao. Wote wanaomkimbilia. Maana ni nani aliye Mungu ila BWANA? Ni nani aliye mwamba ila Mungu wetu? Mungu ndiye anifungaye mshipi wa nguvu, Naye anaifanya kamilifu njia yangu. Miguu yangu anaifanya kuwa ya kulungu, Na kunisimamisha mahali pangu pa juu. Ananifundisha mikono yangu vita, Mikono yangu ikaupinda upinde wa shaba. Nawe umenipa ngao ya wokovu wako, Mkono wako wa kuume umenitegemeza, Na unyenyekevu wako umenikuza. Umezifanyizia nafasi hatua zangu, Na miguu yangu haikuteleza. Nitawafuatia adui zangu na kuwapata, Wala sitarudi nyuma hata wakomeshwe. Nitawapiga-piga wasiweze kusimama, Wataanguka chini ya miguu yangu. Nawe hunifunga mshipi wa nguvu kwa vita, Hunitiishia chini yangu walioniondokea. Naam, adui zangu umewafanya wanipe visogo, Nao walionichukia nimewakatilia mbali. Walipiga yowe, lakini hakuna wa kuokoa, Walimwita BWANA lakini hakuwajibu, Nikawaponda kama mavumbi mbele ya upepo, Nikawatupa nje kama matope ya njiani. Umeniokoa na mashindano ya watu, Umenifanya niwe kichwa cha mataifa. Watu nisiowajua walinitumikia. Kwa kusikia tu habari zangu, Mara wakanitii. Wageni walinijia wakinyenyekea. Wageni nao walitepetea, Walitoka katika ngome zao wakitetemeka. BWANA ndiye aliye hai; Na ahimidiwe mwamba wangu; Na atukuzwe Mungu wa wokovu wangu; Ndiye Mungu anipatiaye kisasi; Na kuwatiisha watu chini yangu. Huniponya na adui zangu; Naam, waniinua juu yao walioniinukia, Na kuniponya na mtu wa jeuri. Basi, BWANA, nitakushukuru kati ya mataifa, Nami nitaliimbia jina lako. Ampa mfalme wake wokovu mkuu, Amfanyia fadhili masihi wake, Daudi na mzao wake hata milele.

Shirikisha
Soma Zaburi 18

Zaburi 18:21-50 Neno: Bibilia Takatifu (NEN)

Kwa maana nimezishika njia za BWANA; sijatenda ubaya nikamwacha Mungu wangu. Sheria zake zote zi mbele yangu, wala sijayaacha maagizo yake. Nimekuwa sina hatia mbele zake, nami nimejilinda nisitende dhambi. BWANA amenilipa sawasawa na uadilifu wangu; sawasawa na usafi wa mikono yangu machoni pake. Kwa yeye aliye mwaminifu, unajionyesha kuwa mwaminifu, kwa asiye na hatia, unajionyesha kutokuwa na hatia. Kwa aliye mtakatifu, unajionyesha kuwa mtakatifu, lakini kwa aliyepotoka, unajionyesha kuwa mkaidi. Wewe huwaokoa wanyenyekevu, lakini huwashusha wenye kiburi. Wewe, Ee BWANA, unaifanya taa yangu iendelee kuwaka; Mungu wangu hulifanya giza langu kuwa mwanga. Kwa msaada wako naweza kushinda jeshi, nikiwa pamoja na Mungu wangu nitaweza kuruka ukuta. Kuhusu Mungu, njia yake ni kamilifu, neno la BWANA halina dosari. Yeye ni ngao kwa wote wanaokimbilia kwake. Kwa maana ni nani aliye Mungu zaidi ya BWANA? Ni nani aliye Mwamba isipokuwa Mungu wetu? Mungu ndiye anivikaye nguvu na kufanya njia yangu kuwa kamilifu. Huifanya miguu yangu kama miguu ya kulungu, huniwezesha kusimama mahali palipo juu. Huifundisha mikono yangu kupigana vita; mikono yangu inaweza kupinda upinde wa shaba. Hunipa ngao yako ya ushindi, nao mkono wako wa kuume hunitegemeza, unajishusha chini ili kuniinua. Huyapanua mapito yangu, ili miguu yangu isiteleze. Niliwafuatia adui zangu na nikawapata, sikurudi nyuma mpaka walipoangamizwa. Niliwaseta hata hawakuweza kuinuka tena; walianguka chini ya miguu yangu. Ulinivika nguvu kwa ajili ya kupigana vita; uliwafanya adui zangu wasujudu miguuni pangu. Uliwafanya adui zangu wageuke na kukimbia, nami nikawaangamiza adui zangu. Walipiga yowe, lakini hapakuwepo na yeyote wa kuwaokoa; walimlilia BWANA, lakini hakuwajibu. Niliwaponda kama mavumbi yanayopeperushwa na upepo; niliwamwaga nje kama tope barabarani. Umeniokoa kutokana na mashambulizi ya watu; umenifanya kuwa kiongozi wa mataifa, watu ambao sikuwajua wananitumikia. Mara wanisikiapo hunitii, wageni hunyenyekea mbele yangu. Wote wanalegea, wanatoka katika ngome zao wakitetemeka. BWANA yu hai! Sifa ni kwa Mwamba wangu! Atukuzwe Mungu Mwokozi wangu! Yeye ndiye Mungu anilipiziaye kisasi, awatiishaye mataifa chini yangu, aniokoaye na adui zangu. Uliniinua juu ya adui zangu; uliniokoa toka kwa watu wajeuri. Kwa hiyo nitakusifu katikati ya mataifa, Ee BWANA; nitaliimbia sifa jina lako. Humpa mfalme wake ushindi mkuu, huonyesha fadhili zake kwa mpakwa mafuta wake, kwa Daudi na wazao wake milele.

Shirikisha
Soma Zaburi 18