Zaburi 123:1-4
Zaburi 123:1-4 Biblia Habari Njema (BHN)
Nakutazamia kwa hamu, ee Mwenyezi-Mungu, nakuangalia wewe utawalaye huko juu mbinguni! Kama watumishi wamtegemeavyo bwana wao, kama mjakazi amtegemeavyo bibi yake, ndivyo nasi tunavyokutegemea wewe, ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, mpaka hapo utakapotuonea huruma. Utuhurumie, ee Mwenyezi-Mungu, utuhurumie, maana tumedharauliwa kupita kiasi. Tumeshiba muda mrefu dharau za matajiri, tumepuuzwa mno na wenye kiburi.
Zaburi 123:1-4 Swahili Revised Union Version (SRUV)
Nimekuinulia macho yangu, Wewe uketiye mbinguni. Kama vile macho ya watumishi Yanavyoutegemea mkono wa bwana zao Kama macho ya mjakazi Yanavyoutegemea mkono wa bimkubwa wake; Ndivyo macho yetu yanavyomtegemea BWANA, Mungu wetu, Hadi atakapoturehemu. Uturehemu, Ee BWANA, uturehemu sisi, Kwa maana tumeshiba dharau. Nafsi zetu zimeshiba mzaha wa wenye raha, Na dharau ya wenye kiburi.
Zaburi 123:1-4 Maandiko Matakatifu ya Mungu Yaitwayo Biblia (SUV)
Nimekuinulia macho yangu, Wewe uketiye mbinguni. Kama vile macho ya watumishi Kwa mkono wa bwana zao Kama macho ya mjakazi Kwa mkono wa bibi yake; Hivyo macho yetu humwelekea BWANA, Mungu wetu, Hata atakapoturehemu. Uturehemu, Ee BWANA, uturehemu sisi, Kwa maana tumeshiba dharau. Nafsi zetu zimeshiba mzaha wa wenye raha, Na dharau ya wenye kiburi.
Zaburi 123:1-4 Neno: Maandiko Matakatifu 2024 (NENO)
Ninayainua macho yangu kwako, kwako wewe unayeketi mbinguni kwenye kiti chako cha enzi. Kama vile macho ya watumwa yatazamavyo mkono wa bwana wao, kama vile macho ya mjakazi yatazamavyo mkono wa bibi yake, ndivyo macho yetu yamtazamavyo Mwenyezi Mungu, Mungu wetu, hadi atakapotuhurumia. Uturehemu, Ee Mwenyezi Mungu, uturehemu, kwa maana tumevumilia dharau nyingi. Tumevumilia dhihaka nyingi kutoka kwa wenye kiburi, dharau nyingi kutoka kwa wenye majivuno.