Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Isaya 7:10-25

Isaya 7:10-25 Biblia Habari Njema (BHN)

Tena Mwenyezi-Mungu akamwambia Ahazi, “Mwombe Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, akupe ishara; iwe ni kutoka chini kuzimu au juu mbinguni.” Ahazi akajibu, “Sitaomba ishara! Sitaki kumjaribu Mwenyezi-Mungu.” Basi, Isaya akamjibu, “Sikiliza basi, enyi watu wa ukoo wa Daudi! Je, haitoshi kuwachosha watu hata sasa mnataka kumchosha Mungu wangu pia? Haya basi, Bwana mwenyewe atawapa ishara: Msichana atachukua mimba, atajifungua mtoto wa kiume na kumwita jina lake Emanueli. Atakula siagi na asali mpaka atakapojua kukataa mabaya na kuchagua mema. Maana, kabla mtoto huyo hajajua kukataa maovu na kuchagua mema, nchi za wafalme hao wawili unaowaogopa zitakuwa mahame. Mwenyezi-Mungu atakuletea wewe pamoja na watu wako na jamii yote ya kifalme siku za taabu kuliko zile zote zilizowahi kutokea tangu wakati watu wa Efraimu walipojitenga na Yuda; yaani, atawaleteeni mfalme wa Ashuru.” Wakati huo, Mwenyezi-Mungu atawapigia mruzi watu wa Misri waje kama nzi toka vijito vya mto Nili; na watu wa Ashuru waje kama nyuki kutoka nchi yao. Watakuja makundi kwa makundi na kuyajaza mabonde yaliyopasukapasuka, mapango miambani, miiba, vichaka vyote na malisho yote. Wakati huo, Bwana atakopa wembe kutoka ngambo ya mto Eufrate, yaani mfalme wa Ashuru. Atawanyoa vichwa vyenu, miili yenu na kukatilia mbali pia ndevu zenu. Wakati huo, mtu atafuga ng'ombe mmoja mchanga na kondoo wawili; nao watatoa maziwa kwa wingi hata aweze kula siagi. Watu watakaosalia katika nchi watakula siagi na asali. Wakati huo, kila mahali palipokuwa na mashamba ya mizabibu kwa maelfu ya thamani ya fedha 1,000 kwa kipimo cha hekalu yatakuwa mbigili na miiba mitupu. Watu watakwenda huko kuwinda kwa pinde na mishale, maana nchi yote itakuwa imejaa mbigili na miiba. Nayo milima yote iliyokuwa ikilimwa itakuwa imejaa mbigili na miiba, hata hakuna mtu atakayejaribu kwenda huko, badala yake itakuwa malisho ya ng'ombe na kondoo.

Shirikisha
Soma Isaya 7

Isaya 7:10-25 Swahili Revised Union Version (SRUV)

Tena BWANA akasema na Ahazi akinena, Jitakie ishara ya BWANA, Mungu wako; itake katika mahali palipo chini sana, au katika mahali palipo juu sana. Lakini Ahazi akasema, Sitaitaka, wala sitamjaribu BWANA. Naye akasema, Sikilizeni sasa, enyi nyumba ya Daudi; Je! Ni neno dogo kwenu kuwachosha wanadamu, hata mkataka kumchosha Mungu wangu pia? Kwa hiyo Bwana mwenyewe atawapa ishara. Tazama, bikira atachukua mimba, atazaa mtoto wa kiume, naye atamwita jina lake Imanueli. Siagi na asali atakula, wakati ajuapo kuyakataa mabaya na kuyachagua mema. Kwa maana kabla mtoto huyo hajajua kuyakataa mabaya na kuyachagua mema, nchi ile, ambayo wewe unawachukia wafalme wake wawili, itaachwa ukiwa. BWANA ataleta juu yako, na juu ya watu wako, na juu ya nyumba ya baba yako, siku zisizokuja bado, tangu siku ile aliyoondoka Efraimu kutoka katika Yuda; yaani, mfalme wa Ashuru. Tena itakuwa katika siku hiyo BWANA atampigia kelele inzi aliye katika pande za mwisho za mito ya Misri, na nyuki aliye katika nchi ya Ashuru Nao watakuja na kutulia katika mabonde yaliyo ukiwa, na katika pango za majabali, na juu ya michongoma yote, na juu ya malisho yote. Katika siku hiyo Bwana atanyoa kichwa na malaika ya miguuni, kwa wembe ulioajiriwa pande za ng'ambo ya Mto, yaani, kwa mfalme wa Ashuru, nao utaziondoa ndevu pia. Katika siku hiyo itakuwa ya kwamba mtu atalisha ng'ombe jike mchanga na kondoo wawili wa kike; kisha itakuwa, kwa sababu wanyama hao watatoa maziwa mengi, atakula siagi; kwa maana kila mtu aliyesalia katika nchi hii atakula siagi na asali. Tena itakuwa katika siku hiyo kila mahali palipokuwa na mizabibu elfu moja, iliyopata fedha elfu moja, patakuwa mahali pa mbigili na miiba tu. Mtu atakayekwenda huko atakwenda na mishale na upinde; kwa sababu nchi yote itakuwa ina mbigili na miiba. Na vilima vyote vilivyolimwa kwa jembe, hutafika huko kwa sababu ya kuiogopa mbigili na miiba, lakini hapo patakuwa mahali pa kupeleka ng'ombe, mahali pa kukanyagwa na kondoo.

Shirikisha
Soma Isaya 7

Isaya 7:10-25 Maandiko Matakatifu ya Mungu Yaitwayo Biblia (SUV)

Tena BWANA akasema na Ahazi akinena, Jitakie ishara ya BWANA, Mungu wako; itake katika mahali palipo chini sana, au katika mahali palipo juu sana. Lakini Ahazi akasema, Sitaitaka, wala sitamjaribu BWANA. Naye akasema, Sikilizeni sasa, enyi nyumba ya Daudi; Je! Ni neno dogo kwenu kuwachosha wanadamu, hata mkataka kumchosha Mungu wangu pia? Kwa hiyo Bwana mwenyewe atawapa ishara. Tazama, bikira atachukua mimba, atazaa mtoto mwanamume, naye atamwita jina lake Imanueli. Siagi na asali atakula, wakati ajuapo kuyakataa mabaya na kuyachagua mema. Kwa maana kabla mtoto huyo hajajua kuyakataa mabaya na kuyachagua mema, nchi ile, ambayo wewe unawachukia wafalme wake wawili, itaachwa ukiwa. BWANA ataleta juu yako, na juu ya watu wako, na juu ya nyumba ya baba yako, siku zisizokuja bado, tangu siku ile aliyoondoka Efraimu kutoka katika Yuda; yaani, mfalme wa Ashuru. Tena itakuwa katika siku hiyo BWANA atampigia kelele inzi aliye katika pande za mwisho za mito ya Misri, na nyuki aliye katika nchi ya Ashuru Nao watakuja na kutulia katika mabonde yaliyo ukiwa, na katika pango za majabali, na juu ya michongoma yote, na juu ya malisho yote. Katika siku hiyo Bwana atanyoa kichwa na malaika ya miguuni, kwa wembe ulioajiriwa pande za ng’ambo ya Mto, yaani, kwa mfalme wa Ashuru, nao utazimaliza ndevu nazo. Katika siku hiyo itakuwa ya kwamba mtu atalisha ng’ombe mke mchanga na kondoo wake wawili; kisha itakuwa, kwa sababu wanyama hao watatoa maziwa mengi, atakula siagi; kwa maana kila mtu aliyesalia katika nchi hii atakula siagi na asali. Tena itakuwa katika siku hiyo kila mahali palipokuwa na mizabibu elfu, iliyopata fedha elfu, patakuwa mahali pa mbigili na miiba tu. Mtu atakayekwenda huko atakwenda na mishale na upinde; kwa sababu nchi yote itakuwa ina mibigili na miiba. Na vilima vyote vilivyolimwa kwa jembe, hutafika huko kwa sababu ya kuiogopa mibigili na miiba, lakini hapo patakuwa mahali pa kupeleka ng’ombe, mahali pa kukanyagwa na kondoo.

Shirikisha
Soma Isaya 7

Isaya 7:10-25 Neno: Bibilia Takatifu (NEN)

BWANA akasema na Ahazi tena, “Mwombe BWANA Mungu wako ishara, iwe kwenye vina virefu sana, au kwenye vimo virefu sana.” Lakini Ahazi akasema, “Sitaomba; sitamjaribu BWANA.” Ndipo Isaya akasema, “Sikia sasa, ewe nyumba ya Daudi! Je, haitoshi kujaribu uvumilivu wa wanadamu? Je, mtaujaribu uvumilivu wa Mungu wangu pia? Kwa hiyo Bwana mwenyewe atawapa ishara: Bikira atachukua mimba, naye atamzaa mwana, na ataitwa Imanueli. Atakula jibini na asali atakapokuwa ameweza kukataa mabaya na kuchagua mema. Lakini kabla mtoto hajajua kukataa mabaya na kuchagua mema, nchi ya wafalme hao wawili unaowaogopa itafanywa ukiwa. BWANA ataleta juu yako, juu ya watu wako, na juu ya nyumba ya baba yako wakati ambao haujawahi kuwako tangu Efraimu alipojitenga na Yuda: yeye atawaleteeni mfalme wa Ashuru.” Katika siku ile BWANA atawapigia filimbi mainzi kutoka vijito vya mbali vya Misri, na nyuki kutoka nchi ya Ashuru. Wote watakuja na kukaa kwenye mabonde yenye miteremko, na kwenye nyufa za miamba, kwenye vichaka vyote vyenye miiba, na kwenye mashimo yote ya maji. Katika siku ile Bwana atatumia wembe ulioajiriwa kutoka ngʼambo ya Mto, yaani mfalme wa Ashuru, kunyoa nywele za kichwa chako na malaika ya miguu yako, na kuziondoa ndevu zako pia. Katika siku ile, mtu atahifadhi hai ndama mmoja na kondoo wawili. Kwa ajili ya wingi wa maziwa watakayotoa, atapata jibini ya kula. Wote watakaobakia katika nchi watakula jibini na asali. Katika siku ile, kila mahali palipokuwa na mizabibu elfu moja yenye thamani ya shekeli 1,000 za fedha, patakuwa na michongoma na miiba tu. Watu watakwenda huko wakiwa na upinde na mshale, kwa maana nchi itafunikwa na michongoma na miiba. Kuhusu vilima vyote vilivyokuwa vikilimwa kwa jembe, hamtakwenda huko tena kwa ajili ya hofu ya michongoma na miiba. Patakuwa mahali ambapo ngʼombe wataachiwa huru, na kondoo kukimbia kimbia.

Shirikisha
Soma Isaya 7

YouVersion hutumia vidakuzi kubinafsisha matumizi yako. Kwa kutumia tovuti yetu, unakubali matumizi yetu ya vidakuzi kama ilivyoelezwa katika Sera yetu ya Faragha