Kumbukumbu la Sheria 8:2-6
Kumbukumbu la Sheria 8:2-6 Biblia Habari Njema (BHN)
Kumbukeni jinsi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, alivyowaongoza katika safari ndefu kupitia jangwani kwa muda wa miaka hiyo arubaini, ili awatweze na kuwajaribu ili ajue mliyokuwa mnawaza mioyoni mwenu, na kama mngezishika amri zake au la. Aliwanyenyekesha, akawaacha muone njaa na baadaye akawapa mana mle, chakula ambacho hamkukijua, wala babu zenu hawajapata kukijua. Alifanya hivyo ili apate kuwafundisha kuwa binadamu haishi kwa mkate tu, bali kwa kila asemalo Mwenyezi-Mungu. Wakati huo wa miaka arubaini nguo zenu hazikuchakaa, wala miguu yenu haikuvimba. Kumbukeni kwamba Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, anawarudi kama vile baba amrudivyo mwanawe. Hivyo, shikeni amri za Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, mpate kuzifuata njia zake na kumcha yeye.
Kumbukumbu la Sheria 8:2-6 Swahili Revised Union Version (SRUV)
Nawe utaikumbuka njia ile yote BWANA, Mungu wako aliyokuongoza miaka hii arubaini katika jangwa, ili akunyenyekeze, kukujaribu kuyajua yaliyo moyoni mwako, kwamba utashika amri zake, au sivyo. Akakunyenyekeza, akakuacha uone njaa, akakulisha kwa mana, usiyoijua wewe wala baba zako hawakuijua; apate kukujulisha ya kuwa mwanadamu haishi kwa mkate tu, bali huishi kwa kila litokalo katika kinywa cha BWANA. Mavazi yako hayakuchakaa, wala mguu wako haukuvimba, miaka hiyo arubaini. Nawe fikiri moyoni mwako, ya kuwa kama vile baba amrudivyo mwanawe, ndivyo BWANA, Mungu wako, akurudivyo. Nawe uzishike amri za BWANA, Mungu wako, upate kwenda katika njia zake, na kumcha.
Kumbukumbu la Sheria 8:2-6 Maandiko Matakatifu ya Mungu Yaitwayo Biblia (SUV)
Nawe utaikumbuka njia ile yote BWANA, Mungu wako aliyokuongoza miaka hii arobaini katika jangwa, ili akutweze, kukujaribu kuyajua yaliyo moyoni mwako, kwamba utashika amri zake, au sivyo. Akakutweza, akakuacha uone njaa, akakulisha kwa mana, usiyoijua wewe wala baba zako hawakuijua; apate kukujulisha ya kuwa mwanadamu haishi kwa mkate tu, bali huishi kwa kila litokalo katika kinywa cha BWANA. Mavazi yako hayakuchakaa, wala mguu wako haukuvimba, miaka hiyo arobaini. Nawe fikiri moyoni mwako, ya kuwa kama vile baba amrudivyo mwanawe, ndivyo BWANA, Mungu wako, akurudivyo. Nawe uzishike amri za BWANA, Mungu wako, upate kwenda katika njia zake, na kumcha.
Kumbukumbu la Sheria 8:2-6 Neno: Bibilia Takatifu (NEN)
Kumbuka jinsi BWANA Mungu wenu alivyowaongoza katika njia yote katika jangwa kwa miaka hii arobaini, kukunyenyekeza na kukujaribu ili ajue lililoko moyoni mwako, kwamba utayashika maagizo yake au la. Alikudhili na kukufanya uone njaa kisha akulishe kwa mana, ambayo wewe wala baba zako hamkuijua, awafundishe kuwa mwanadamu hataishi kwa mkate tu bali kwa kila neno litokalo katika kinywa cha BWANA. Nguo zenu hazikuchakaa wala miguu yenu haikuvimba kwa miaka hii arobaini. Mjue basi ndani ya mioyo yenu kama mtu anavyomwadibisha mwanawe, ndivyo BWANA Mungu wako atawaadibisha ninyi. Shikeni maagizo ya BWANA Mungu wenu mtembee katika njia zake na kumheshimu.