Ezekieli 28:11-15
Ezekieli 28:11-15 BHN
Tena neno la Mwenyezi-Mungu lilinijia: “Wewe mtu! Imba wimbo wa maombolezo juu ya mfalme wa Tiro. Mwambie kuwa mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Wewe mfalme wa Tiro ulikuwa upeo wa ukamilifu; ulijaa hekima na uzuri kamili. Ulikaa Edeni, bustani ya Mungu. Ulipambwa kwa kila namna ya johari, akiki, topazi, yaspi, zabarajadi, berili, sardoniki, johari ya rangi ya samawati, almasi na zumaridi. Ulikuwa na mapambo ya dhahabu. Yote uliwekewa tayari siku ulipoumbwa. Nilimteua malaika kukulinda, uliishi katika mlima wangu mtakatifu na kutembea juu ya vito vinavyometameta. Uliishi maisha yasiyo na lawama, tangu siku ile ulipoumbwa, hadi ulipoanza kufanya uovu.