Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Yohana 11:28-46

Yohana 11:28-46 NENO

Baada ya kusema haya, Martha alienda akamwita Mariamu dada yake faraghani na kumwambia, “Mwalimu yuko hapa anakuita.” Mariamu aliposikia hivyo, akaondoka upesi, akaenda hadi alipokuwa Yesu. Yesu alikuwa hajaingia kijijini, bali alikuwa bado yuko mahali pale alipokutana na Martha. Wale Wayahudi waliokuwa pamoja na Mariamu nyumbani wakimfariji walipoona ameondoka haraka na kutoka nje, walimfuata wakidhani kwamba alikuwa anaenda kule kaburini kulilia huko. Mariamu alipofika mahali pale Yesu alipokuwa, alipiga magoti miguuni pake na kusema, “Bwana, kama ungekuwa hapa, ndugu yangu hangekufa.” Yesu alipomwona Mariamu akilia na wale Wayahudi waliokuja pamoja naye pia wakilia, Yesu alisikia uchungu moyoni, akafadhaika sana. Akauliza, “Mmemweka wapi?” Wakamwambia, “Bwana, njoo upaone.” Yesu akalia machozi. Ndipo Wayahudi wakasema, “Tazama jinsi alivyompenda Lazaro!” Lakini wengine wakasema, “Je, yule aliyefungua macho ya kipofu, hakuweza kumfanya na huyu asife?” Yesu akafika penye kaburi akiwa amefadhaika sana kwa mara nyingine. Hilo kaburi lilikuwa pango ambalo jiwe liliwekwa kwenye ingilio lake. Yesu akasema, “Liondoeni jiwe.” Martha dada yake yule aliyekuwa amekufa akasema, “Lakini Bwana, wakati huu atakuwa ananuka kwani amekwisha kuwa kaburini siku nne.” Yesu akamwambia, “Sikukuambia kwamba ukiamini utauona utukufu wa Mungu?” Kwa hiyo wakaliondoa lile jiwe kutoka kaburini. Yesu akainua macho yake juu, akasema, “Baba, ninakushukuru kwa kuwa wanisikia. Ninajua ya kuwa wewe hunisikia siku zote, lakini nimesema haya kwa ajili ya watu hawa waliosimama hapa, ili wapate kuamini ya kuwa wewe umenituma.” Baada ya kusema haya, Yesu akapaza sauti yake, akaita, “Lazaro, njoo huku!” Yule aliyekuwa amekufa akatoka nje, mikono yake na miguu yake ikiwa imeviringishiwa vitambaa vya kitani na leso usoni pake. Yesu akawaambia, “Mfungueni; mwacheni aende zake.” Hivyo Wayahudi wengi waliokuwa wamekuja kumfariji Mariamu walipoona yale Yesu aliyoyatenda, wakamwamini. Lakini baadhi yao wakaenda kwa Mafarisayo na kuwaambia mambo Yesu aliyoyafanya.